Usafi uwe wa kudumu, usiwe kwa sikukuu tu

 


 

Salum Vuai Issa ( Muhenga)

Na Salum Vuai

 

KATIKA uzinduzi wa ‘Wiki ya Dk. Hussein Mwinyi’ Jumatatu Novemba mosi ikiwa sehemu ya maadhimisho ya kutimiza mwaka mmoja wa uongozi wake, wananchi sote tulihamasika kusafisha miji na mitaa yetu ili ipendeze.

 

Ukiachia Mkoa wa Kusini Unguja na Kaskazini Pemba ambako zoezi hilo la usafi lilifanyika kitaifa, wananchi katika shehia mbalimbali walionesha mshikamano mkubwa kuhakikisha nchi inakuwa safi.

 

Aidha, kwa mujibu wa Mwenyekiti wa kamati ya maadhimisho hayo Idrissa Kitwana Mustafa ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi, wito wa kufanya usafi ni utekelezaji wa kauli ya mara kwa mara ya Rais Dk. Mwinyi kutaka tuipendezeshe nchi yetu kwa kuisafisha.

 

Kwa hakika uchafu una madhara makubwa kiafya na pia unatoa taswira mbaya kwa watalii na wageni wengine wanaotutembelea, wakati Zanzibar ni miongoni mwa visiwa vinavyovutia utalii ambao kwa sasa ndio chanzo kikuu cha kuiingizia nchi mapato.

 

Kama ilivyo desturi na utamaduni wa Wazanzibari unapofika msimu wa sikukuu kusafisha na kupamba nyumba zao kwa samani mpya, mapazia na mavazi, ndivyo inavyopasa kufanya hivyo kwa nchi.

 

Wazanzibari wa itikadi zote za dini wamejenga utamaduni huu wa kujipamba siku za sikukuu lakini Muhenga katika tafakuri yake anauona ni mzuri.

 

Hata hivyo, utamaduni huu unafaa kuendelezwa hata kusipokuwa na sherehe au maadhimisho ya tukio lolote kubwa la kijamii au kitaifa.

 

Itakuwa aibu kama baada ya kuhitimisha sherehe za kumpongeza Rais, kuona taka na uchafu wa karo zinazofurika unarudi tena mitaani.

 

Nimelazimika kutoa tanbihi hii kwani imekuwa mazoea miongoni mwa wananchi, kuwa wazuri wa kufuata maelekezo ya wataalamu wa afya wakati wa dharura tu mathalan kunapokuwa na maradhi ya mripuko.

 

Mara tu baada ya kudhibitiwa kwa maradhi ya kuambukiza ikiwemo kipindupindu, watu hupuuza kuchukua tahadhari na kurudi katika mazoea ya kula na kunywa bila kufuata masharti ya kiafya ikiwemo kuchemsha maji.

 

Katika jambo hili, kwanza kila siku tuhakikishe mazingira ya ndani na nje kwa kila kaya yanasafishwa vizuri, takataka zinachomwa moto na zile zisizochomeka zikusanywe ili wenye dhamana wapite kuzichukua.

 

Aidha chini ya usimamizi wa masheha na kamati zao, kuwekwe utaratibu kwa wakaazi wa mitaa kushirikiana kusafisha maeneo yao angalau kila siku moja ya mwisho wa wiki.

 

Utaratibu huu uwe mbali na ule usafi wa kitaifa kila mwisho au mwanzo wa mwezi ambao huko nyuma ulikuwa ukitekelezwa kila wilaya.

 

Kamwe Muhenga hatarajii zoezi la usafi lililofanyika mwanzoni mwa wiki iwe njia ya kujikweza tu kwa mkuu wa nchi kisha watu warudi katika tabia mbaya ya kutupa taka kila pahala.

 

Aidha, jamii ihamasishwe kutumia karo kwa ajili ya kuhifadhi maji machafu yatokayo majumbani mwao, badala ya kuyamwaga mitaani kupitia tobo wanazotoboa kwa kisingizio cha kuepuka karo zao kujaa.      

 

Haipendezi kuwa katika mitaa kuna masheha na madiwani, lakini wanaona muhali kuwachukulia hatua watu wanaotiririsha maji machafu nje ya nyumba zao, jambo linalosababisha tope na harufu mbaya kuhanikiza.  

 

Kwa hivyo, tunapomaliza kuadhimisha mwaka mmoja wa uongozi wa Rais Dk. Hussein Mwinyi, tuhakikishe usafi hauondoki na sherehe hizo kwa watu kuendelea kupuuza umuhimu wa kuyatunza maeneo yao.

 

Kufanya hivyo itakuwa istihizai ambayo itatusuta wenyewe kwa kauli zetu kwamba tunampenda sana Mheshimiwa Rais na kuikubali kasi ya utendaji wake katika kuiletea nchi yetu maendeleo.

 

Simu: 0777 865050/0714 425556

Baruapepe: mbumbwinihalisi@gmail.com

About mmedia

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 Comments:

Post a Comment