Makamu wa Kwanza Rais Zanzibar ataka kuazishwe chombo cha kisheria Dhidi ya Majaa.

 

Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar Othman Masoud Othman




MAKAMU wa kwanza wa Rais wa Zanzibar   Othman Masoud Othman, amesema ni muhimu  Zanzibar kuwa na Chombo rasmi chenye uwezo  na mamlaka ya kisheria  kusimamia masuala  yanayohusu majaa na taka za aina mbali mbali zinazozalishwa kwenye maeneo tofauti nchini yakiwemo mahospitali.

 

Mhe. Makamu ameyasema hayo leo Ofisini kwake Migombani Mjini Zanzibar, katika kikao maalum cha muendelezo wa tathmini  ya ziara yake ya Kimazingira ya hivi karibuni, kilichowashirikisha watendaji wa Jiji la Zanzibar, Manispaa , Mmalaka ya Usimamizi Mazingira  na wa Wizara ya Nchi Afisi ya Rais Tawala za Mikoa na Idara Maalum za SMZ.

 

Makamu amesema pamoja na  serikali kutumia zaidi ya shilingi 21 bilioni, kufanya uwekezaji mkubwa wa  ujenzi wa miundombinu ya jaa la Kisasa huko Kibele, kutupa taka na kulinda mazingira, lakini jaa hilo halitumiki ipasavyo kutokana na kuwepo changamoto ya rasilimali watu na bajeti ya uendeshaji na hivyo kuelekea kutofikiwa matarajio ya jaa hilo.

 

  Amefahamisha kwamba hatua ya kuwa na chombo cha aina hiyo ni muhimu kwa kusaidia Zanzibar kuweka mfumo bora na sahihi zaidi katika hatua za ukusanyaji wa taka, usafirishaji na usimamizi utakaokidhi haja na matarajio kwa hali ya sasa na ya baadae katika utunzaji wa mazingira.

 

Amesema  jaa la kibele lina mfumo bora wa kitaalamu katika kusimiamia na kutenganisha taka za aina mbali mbali pamoja na uwezo wa kuzalisha bidhaa kama vile mbolea, lakini baadhi ya vifaa vilivyopo ambavyo ni vya gharama kubwa  havitumiki kwa sababu mbali mbali jambo linalotishia kutofikiwa matarajio ya kujengwa jaa hilo.

 

Aidha amesema  jaa la kibele ni miongoni mwa majaa ya kisasa na limeigharimu serikali kiasi kubwa cha fedha, lakini iwapo hakutakuwa na chombo chenye jukumu rasmi la usimamizi wa taka, ujezi huo hautakuwa na maana yoyote katika kuweka usafi na utunzaji wa mazingira  nchini.

 


Othman pia katika kikao hicho aliagiza mamlaka zinazohusika na usimamizi wa jaaa hilo kuhakikisha   wanaweka mipango   bora na kutatua kwa haraka baadhi ya changamoto zilizopo ikiwemo uhaba raslimali watu na mafuta ya kuendeshea baadhi ya mitambo ya jaa hilo.

 

Naye meneja wa jaa  la Kibele ndugu Hassan Mohammed Ali, amesema,  Kibele ni miongoni mwa majaa bora Afrika, lakini linakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo baadhi ya vifaa kutotumika hadi sasa, kutupwa baadhi ya taka hatarishi zikiwemo za hospitali  licha kwamba kitaalam hazipaswii kutupwa  katika eneo hilo kwa vile zinaweza kuleta madhara makubwa  kwa binaadamu.

 

Aidha alisema kwamba  pia Zanzibar inakabiliwa na tatizo la ukosefu wa taarifa rasmi za taka , ambapo hadi sasa hakuna taarifa  za uhakika zinazochambua na kuainisha takwimu na kiwango halisi cha taka kinachozalishwa kila siku nchini.

 

Kaimu Waziri wa Nchi, Afisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Dk.  Khalid Salum Mohammed, amesema kwamba kuna haja ya kufikiria zaidi matumizi sahihi ya jaa hilo hasa kwa kuwa limeigharimu serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kiwango kikubwa cha fedha.

 

Amesema kunahitajika muongozo rasmi wa kisera na kiseheria utakaosaidia kuchambua na kuainisha taka zinazotoka katika maeneo mbali mbali  ikiwa ni pamoja na kuwepo mkakati bora wa usimamizi wa taka hizo hapa Zanzibar.

 

Naye Meya wa Jiji la Zanzibar Mstahiki Mahmoud Mohammed Mussa, amekiri kwamba taka za hospitali pamoja na kwamba ni hatarishi, lakini zinaendelea kutupwa katika eneo hilo kutokana na vifaa vya kuchomea taka za aina hiyo katika Hosptali ya Mnazi mmoja kuharibika mara kwa mara.

 

Amesema kutokana na changamoto mbali mbali za usimamizi wa masuala ya taka katika jaa hilo la Kibele, Baraza la Jiji linaendelea na mazungumzo na muekezaji atakayepewa dhamana ya kusimamia masuala ya taka ili  kupata suluhu ya tatizo hilo hapa Zanzibar.

 

About mmedia

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 Comments:

Post a Comment