![]() |
| Baadhi ya wanawake walioshiriki mkutano Tumbe Wilaya Micheweni Pemba wa kampeni dhidi mwanamke kushiriki katika uongozi |
PEMBA
WANANCHI wametakiwa kushirikiana katika kuwainua mwanamke, ili kuhakikisha wanakuwa viongozi kuanzia ngazi
ya jamii hadi Taifa.
Akizungumza na wananchi wa shehia ya
Tumbe Magharibi, Mkurugenzi wa Jumuiya ya PEGAO Pemba Hafidh Abdi Said alisema,
wanawake wao uwezo wa kuongoza na kuleta mabadiliko ya haraka, hivyo ni vyema
jamii ikampa mashirikiano katika kuusaka uongozi.
Alisema, katika jamii kuna vikundi
na Jumuiya mbali mbali zinazoanzishwa kwa ajili ya kuleta maendeleo, ingawa
kinachomshangaza ni kuona kuwa wanawake hunyimwa hata nafasi hizo, jambo ambalo
sio sahihi kwani wanawafanya waendelee kubaki nyuma kila siku zinaposonga
mbele.
"Tumekuwa tukiwanyima wanawake
nafasi hata hizi za Jumuiya ndogo ndogo tunazoziunda kwenye jamii, sasa
tunataka tumuinue mwanamke ili na yeye awe kiongozi kwani wanaweza na wanaleta
mabadiliko makubwa", alisema Mkurugenzi huyo.
Aidha aliwataka akinababa kuwaunga
mkono akinamama wanaotia nia ya kugombea uongozi, kwani kila mmoja anamtegemea
mwenzake katika harakati mbali mbali za kijamii, kisiasa na kiuchumi katika
kufikia malengo.
"Sote tunategeneana katika
mambo yetu, hivyo basi tuache kumdharau mwanamke kwamba hawezi wakati huko
nyumbani akiamua baba asifanikiwe basi huwezi kufika pahala, kwa hiyo tujue
kwamba na wao wana mchango mkubwa", alisema.
Akiwasilisha mada katika mkutano huo
Mudathir Sharif Khamis alisema, kuwa kila mmoja yuko sawa mbele ya Sheria,
hivyo si vyema kumnyima mwanamke kugombea uongozi kwa kisingizio cha kuwa yeye
ni mama wa nyumbani.
"Akinababa tusiwabane wanawake,
wapo viongozi wanawake ambao wanaongoza na wanaleta mabadiliko makubwa katika
jamii yetu", alisema Mudathir.
Nae muwasilishaji Hadia Sultan Hamad
alieleza, kuna baadhi ya wanajamii humkwamisha mwanamke katika kugombea nafasi
hizo kwa kisingizio cha dini, jambo ambalo so sahihi kwani zamani walikuwepo
wanawake wa kiislamu ambao walikuwa wakisimamia mambo mbali mbali katika jamii
zao.
"Tuwaelimishe watoto wetu wa
kike tangu wakiwa skuli na kuwaelekeza kwamba na wao wanayo haki ya kugombea
uongozi, ili watakapofikia muda wasione ajabu na badala yake wawe mstari wa
mbele katika hili", alisema.
Kwa upande wake Maryam Hemed Said
mkaazi wa Tumbe alieleza kuwa, wanawake ambao ni viongozi wameleta mchango
mkubwa katika jamii na juhudi mbali mbali zinaonekana katika kuliletea Taifa
maendeleo.
"Miaka ya hivi karibuni baada
ya wanawake kuanza kuwa viongozi imeonekana wametoa mchango mkubwa na juhudi
zao zinaonekana kwani wamefanya mambo mengi ambayo hata hao wanaume
hawakuyafanya", alifafanua.
Akichangia katika mkutano huo Ali
Mohamed Bakar alisema kuwa, wanawake wanashindwa kufikia uongozi kutokana na
mifumo ya kiutawala iliyopo katika vyama, kwani huwekewa vizingiti vikubwa.
"Wakati mwengine utaona kwamba
mwanamke anapata nafasi ya pili katika watu tisa waliogombea na wote aghalabu
huwa ni wanaume, kwanini tusimpe kipaombele kwa pale kwa ujasiri wake
aliouonesha, vyama vibadili mifumo yao na vimpe nafasi mwanamke", alisema.
"Unakitumikia chama usiku
mchana baadae siku za kugombea anatokea mwenye pesa anawapa watu, hivyo hapa
wanawake wengi hushindwa kwa sababu hawana pesa, jambo ambalo linawasababishia
kuvunjika moyo, ila nawashauri wasirudi nyuma", alifahamisha.
Kwa upande wao wananchi wengine
walisema kuwa, kumekuwa na viongozi kwenye majimbo ambao huwashawishi wapiga
kura wasimpe mwanamke na kuwabandikiza chuki zisizo na sababu, jambo ambalo
linawaumiza sana wanaogombea.

0 Comments:
Post a Comment