| Picha na Maktaba |
PEMBA
WAFANYABIASHARA
ya saruji wametakiwa kuuza bidhaa hiyo kwa mujibu wa bei elekezi ambayo
imewekwa na Serikali ya Zanzibar.
Akizungumza baada ya
ukaguzi wa maduka ya saruji kwa Wilaya zote za Pemba, Mkurugenzi wa Kumlinda mtumiaji
na Umiliki wa bidhaa bandia Zanzibar Aaliye Emanuel Juma alisema, wafanyabiashara
wamekuwa wakifanya ubadhirifu kwa bidhaa ya saruji licha ya bei Serikali kuweka
bei elekezi.
Alisema kuwa, Tume ya
Ushindani halala wa Biashara inawataka wafanyabiashara hao kufuata maagizo ya Serikali
kwa kuuza bidhaa hiyo kwa mujibu wa bei iliyowekwa kisheria.
Alieleza kuwa, zoezi
hilo walilifanya baada ya kuona kwamba baadhi ya wafanyabiasha sio waaminifu,
ambapo wamepandisha bei kwa bidhaa hiyo ya saruji mpaka kufikia shilingi 20,000/=
jambo ambalo ni kosa.
“Kwa mujibu wa sheria
namba 5 ya mwaka 2018 Tume ya ushindani halala wa Biashara imeweka bei elekezi
kwa bidhaa hiyo, hivyo ipo haja ya wafanyabiashara kuifuata”, alisema
Mkurugenzi huyo.
Mkurugenzi huyo
alifahamisha kuwa, Serikali imeangalia gharama zote za usafirishaji wa biadhaa
hiyo na ndipo ikaweka bei elekezi kwa wafanyabiashara hao, kwani wamekuwa
wakiwaumiza wananchi.
“Saruji zinazotoka
Tanzania bara ambayo ni samba, dangote na twiga inatakiwa kuuzwa kwa shilingi
16,500 na kwa ile saruji inayotoka Omani inatakiwa kuuzwa kwa shilingi 19,000
kwa upande wa Pemba”, alisema.
Aliwataka
wafanyabiashara hao kufika Wizara husika ikiwa kuna tatizo, ili waweze kukaa
pamoja na kulitatua kwani wanataka wananchi wapate biadhaa kwa mujibu stahiki kama
ilivyoelekeza Serikali na sio kuwakomoa.
Aidha Mkurugenzi huyo
alisema kuwa, wakati wa ukaguzi huo waligundua kuwa, hakuna mfanyabiashara
yeyote ambae amebandika bei katika bidhaa yake.
“Kwa mujibu wa kifungu
cha 59 cha sheria ya tume hiyo, kila mfanyabiashara anatakiwa abandike bei stahikiu
kwa kila bidhaa ili kuepusha udanganyifu, kwani wengine huangalia sura ya mtu
na ndipo wakatoa bei wanayotaka”, alisema Mkurugenzi.
Kwa upande wao
wafanyabiashara wa bidhaa hiyo walisema kuwa, kuna saruji nyengie wanaweza
kuuza kwa bei iliyowekwa na Serikali, ingawa kampuni nyengine hawawezi kutokana
na bei kuwa kubwa.
“Saruji ya Tanga
simenti hatuwezi kuuza kwa bei iliyowekwa na Serikali, kwani tutapata hasara
kubwa, hivyo bora tufunge maduka”, walisema wafanyabiashara hiyo.
Wakala wa saruji ya
Tanga simenti Ali Mohamed Juma mkaazi wa Wete alisema, Serikali imeweka bei
elekezi kwa bidhaa ya saruji ingawa kwa upande wao haiwezekani kuuza hivyo, kwani
watapata hasara kubwa.
“Saruji nyengine
zinazotoka Tanzania bara tunaweza kuuza hata chini ya shilingi 16,000 /= lakini
kwa hii ya Tanga simenti ambayo tunainua kwa shilingi 15,500/=, hatuwezi kuuza
kwa bei iliyowekwa na Serikali kwa sababu gharama zetu hazitorudi”, alisema.
“Mwanzo niliuliza
Wizara kuwa nifunge duka ama niache, kwani kwa bei hiyo siwezi kuendelea,
waliniruhusu kuuza lakini leo wanakuja kunifungia duka, sijui niwaelewe vipi”,
alieleza wakala huyo.
Mfanyabiashara ambae
hakutaka jina lake litajwe alisema kuwa, katika bandari ya Wete wamekuwa
wakilipa kodi sita, hivyo kwa saruji ya Tanga simenti hawawezi kuuza kwa bei
hiyo.
Zoezi la ukaguzi wa
bidhaa ya saruji limefanyika baada ya kuonekana wafanyabiashara kuuza kwa bei
ya juu hadi kufikia shilingi 20,000/= jambo ambalo sio sahihi, ambapo Tume hiyo
imefungia baadhi ya maduka.
0 Comments:
Post a Comment