![]() |
| Waziri wa Nchi Afisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar Sada Mkuya Salum |
Na Raya Hamad - OMKR
Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Mhe Dkt Saada
Mkuya Salum amezishauri taasisi za Serikali na binafsi zinazotoa huduma kwa
jamii kutoa kipaumbele kwa Watu wenye mazingira maalum wakiwemo wenye
Ulemavu wa Uziwi.
Dkt Saada ameyasema hayo wakati akiyafungua mafunzo maalum ya
lugha ya alama kwa watendaji wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii ZSSF yaliyoaandaliwa
na Baraza la Taifa la Watu wenye Ulemavu katika ukumbi wa ZSSF Kariakoo.
Ameipongeza ZSSF kwa kuwa mfano bora kwa mashirika ya serikali
kuonesha kwa vitendo na dhamira njema ya kuwahudumia wananchi wa makundi yote
kwa kuanza na lugha ya alama ambayo itawasaidia viziwi kupata huduma
wanazozitoa kwa uhakika bila ya gharama ya kutafuta mkalimali.
Aidha Dkt Saada ameiomba ZSSF wasiishie hapo bali kutafuta na
njia nyengine ya kuwasaidia Watu wenye Ulemavu wa Uoni kwa kuangalia uwezekano
wa kutengeneza kadi za ZSSF zenye alama ya nukta nundu.
“Naziomba na taasisi za Serikali ili tuwe na jamii shirikishi
basi sasa hata vitabu vya sera na sheria na vyenginevyo tuhakikishe tunaandika
kwa nukta nundu ili wenzetu wenye Ulemavu wa Uoni nao waweze kusoma maendeleo
ya nchi yetu mfano nzuri tulivyoanza Ofisi ya Mkamu wa Kwanza wa Rais Bajeti ya
Serikali tuliwazingatia kwa kutoa vitabu vilivyoandikwa kwa kutumia nukta
nundu”
Kufanya hivyo kutahusisha huduma wanazozitoa kuwa bora zaidi na
zinazokwenda na wakati huu wa ukuwaji wa teknologia pamoja na kuziomba taasisi
nyengine kujipanga ili ziweze kutoa huduma kwa ufanisi bila ya kuwaacha wengine
kama Watu wenye Ulemavu .
Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais kupitia Baraza la Watu wenye
Ulemavu linatambua kuwa fursa mpya ya uchumi wa buluu ni kwa ajili ya maendeleo
ya wananchi wote wa Zanzibar hivyo imejipanga kuandaa mpango mkakati wa kuona
lugha ya alama inapewa kipaumbele kufundishwa kwenye taasisi zote zinazotoa
huduma kwa jamii.
Nae Mkurugenzi wa Baraza la Watu wenye Ulemavu Mhandisi Ussy
Khamis Debe amesema mafunzo ya lugha ya alama yameanzishwa baada ya kuonekana
kuna upungufu kwa taarifa kwa Watu wenye Ulemavu wa Uziwi.
Mhandisi Ussy amesema kati ya changamoto wanazozipata Watu wenye
Ulemavu wa uziwi kutopata taarifa sahihi kwa wakati muafaka na ndio maana
Baraza la Taifa la Watu wenye Ulemavu likaamua kuendelea kutoa elimu hii ya
lugha ya alama kwa taasisi tofauti.
Mafunzo kama hayo pia hutolewa na Jumuiya ya wakalimani wa lugha
ya alama JUWALAZA, Chama cha Viziwi Zanzibar CHAVIZA na chuo cha SUZA, hii ni
awamu ya pili ya muendelezo wa mafunzo ya lugha ya alama kwa Mfuko wa Hifadhi
ya Jamii Zanzibar.

0 Comments:
Post a Comment