Wafanyabiashara Pemba wafurahishwa na Rais Mwinyi



RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akikata utepe kulifungua jengo jipya la Bodi ya Mapato Zanzibar.(ZRB) lilioko katika eneo la Gombani Wilaya ya Chakechake Pemba na (kulia kwa Rais) Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mariam Mwinyi, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya (ZRB) Bw.Saleh Sadiq na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Fedha na Mipango Zanzibar Mhe.Jamal Kassim Ali na (kushoto kwa Rais) Mkuu wa Mkoa wa Kusini Pemba 


 NA ZUHURA JUMA, PEMBA

WAFANYABIASHARA kisiwani Pemba wamemshukuru Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi  Dk Hussein Ali Mwinyi kwa kauli yake aliyoitoa ya kujengwa bandari ya kisasa Mkoani Pemba, ambayo itasaidia meli za mizigo kufika moja kwa moja.

Hivi karibuni Dk: Mwinyi alikuwa na ziara ya siku nne kisiwani Pemba, ambapo alitembelea miradi mbali mbali pamoja kuzungumza na wananchi wa mikoa wilaya nne kusikiliza kero zao.

Katika ziara yake hiyo Dk Mwinyi aliwashukuru wananchi kwa kumchagua kuiongoza Zanzibar ambapo aliwaahidi wananchi kuwatekelezea mambo mbali mbali, ili kuhakikisha nchi inapata maendeleo endelevu.

Wakizungumza na waandishi wa habari hizi kwa nyakati tofauti wafanyabiashara hao walisema kuwa, wamefarijika sana kusikia kauli hiyo ya raisi kutaka kujenga bandari, kwani wanaamini gharama za bidhaa zitapungua kwa kiasi kikubwa.

Walisema kuwa, bidhaa zinapofika kisiwani Pemba zinakuwa ghali sana hali ambayo inasababisha wananchi kushindwa kununua na hatimae kukaa muda mrefu bila kupata wateja.

Walisema kuwa, ikiwa itajengwa bandari ya kisasa, itasaidia meli za mizigo kuja moja kwa moja kisiwani Pemba, hivyo wanaamini kwamba bei ya bidhaa itashuka na kuwapa wafanyabiashara na wananchi ahuweni.

“Bidhaa tunachukua Dar-es-Salaam au Unguja, kwa hiyo tunapofika Pemba bei lazima iwe kubwa kwa sababu kila tunapopita tunalipia mzigo na ukiangalia pia tunatakiwa tulipe kodi, hivyo lazima tuongeze bei ili na sisi tujilipe gharama zetu”, walisema wafanyabiashara hao.

Mfanyabiashara wa kanga na madira Chake Chake Mbarouk Mohamed Zahor alisema, kauli ya dk: Mwinyi kutaka kujenga bandari Mkoani Pemba ni nzuri na anaifagilia sana, kwani anaamini watapata maendeleo mazuri kwao na wananchi kama walivyo wenzao wa nje ya kisiwa hiki.

Alisema kuwa, wanaiunga mkono kauli hiyo kwa asilimia mia kutokana na kuwa itawasaidia sana kupungua kwa gharama za usafirishaji na wananchi watafaidi kwa bei kupungua.

“Biashara kwa Pemba muda mwingi ni ngumu, lakini hii inasababishwa na kuwa bei ni kubwa na pia mizigo huchelewa kupatikana, hivyo ikiwa itajengwa bandari ya kisasa na mizigo kuja Pemba itakuwa ni chachu ya maendeleo yetu kwa kweli”, alisema baba huyo.

Kwa upande wake mfanyabiasha wa nguo za watoto Maulid Ali Kassim alisema, wamefarajika sana walipomsika rais kuhusu kutaka kuijenga bandari, kwani ushuru utapungua kwa kiasi fulani ukilinganisha na wanapochukua nje ya Pemba.

“Ushuru ukipungua na bei zitapungua, hivyo itakuwa ni rahisi kwa wananchi kununua bidhaa zetu, kwa sababu tukinunua kitu shilingi elfu 15,000 huku kinaweza kufika hata shilingi 20,000, hivyo tunawaumiza wananchi hasa wa  kipato cha chini”, alisema.

Maulid alieleza kuwa, kwa sasa biashara ipo vizuri kiasi kutokana na kuwa ni msimu wa karafu, hivyo angalau watu wanapata pesa za kujikimu, lakini utakapomalizika msimu tu biashara huwa ni ngumu sana kwa sababu bei ni ghali sana.

Nae mfanyabiashara wa vitambaa Yussuf Abrahman Mohamed alieleza kuwa, kauli ya dk Mwinyi ni nzuri sana na wanaiunga mkono na kuiomba Serikali kuharakisha kuijenga bandari hiyo, ili kuwasaidia katika shughuli zao za kibiashara.

“Tutapata mafanikio makubwa ikiwa bandari itajengwa ya kisasa na itakuwa ni jambo la busara sana, kwa sababu kila tunapopita lazima tulipie mzigo, hivyo inatugharimu sana na ndio maana bei zinakuwa kubwa”, alisema.

Alimshukuru dk Mwinyi kwa kauli yake hiyo, kwani ni kilio chao cha muda mrefu, hivyo ipo haja ya kuharakishwa jambo hilo, ili kuleta manufaa kwa wafanyabiashara na wananchi kwa ujumla.

Mfanyabiashara ambae hakutaka jina lake litajwe alisema kuwa, wanataka wauze bidhaa kwa bei ndogo kama wenzao wa Unguja na Dar-es-Salaam, lakini wanashindwa kutokana na kuwa wanatumia gharama nyingi kusafirisha hadi kufikia Pemba.

“Wananchi hawatuamini kama tunatumia gharama kubwa mno kuleta bidhaa Pemba na ndio maana wanapokuja madukani wanalalamikia bei kubwa, ila naamini kutokana na kauli ya Dk Mwinyi watafaidika hivi karibuni, kwani bidhaa zitakuwa bei rahisi”, alisema dada huyo.

Mfanabishara Ali Omar Juma amesema kauli iliyotolea na rais kuhusu kujengwa badari itakayoweza kuegesha meli za mizigo kutoka moja kwa moja nchi za nje ni zuri kwao kwani itaweza kuwapunguzia gharama za bidhaa.

“Iwapo bidhaa zitakuja moja kwa moja gharama zitakuwa nafuu, meli zote huishia Unguja ambapo hupata gharama kubwa za usafirishaji na kuweza kusababisha kupata gharama kubwa mteja wa mwisho”, alisema.

Alieleza kuwa, anazidi kumuombea rais azidi kuwa na moyo wa kuwasaidia ili waweze kundokana na changamoto zinazowakabili kwenye biashara zao.

About mmedia

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 Comments:

Post a Comment