![]() |
| Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Pemba Salama Mbarouk Khatib akizungumza katika Ziara yakeWizara ya Habari, Vijana, Sanaa na Mchezo na Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale kwa Mkoa wa Kaskazini Pemba |
MKUU wa Mkoa Kaskazini Pemba Salama Mbarouk Khatib amesema, hakuridhika
na mradi wa kiwanja cha mpira Kishindeni Wilaya ya Micheweni kutokana na
matumizi ya fedha iliyotumika kutokuwa sahihi.
Alisema kuwa, kiwanja
hicho kimegharimu fedha taslimu shilingi milioni 236, ingawa haziendani na
matumizi hayo, jambo ambalo lilimuhuzunisha sana, kwani fedha zinazotumika
kufanyia miradi ya kimaendeleo ni kodi za wananchi.
Akizungumza wakati wa
ziara yake ya kukagua miradi ya maendeleo kwa Wizara ya Habari, Vijana, Sanaa
na Mchezo na Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale kwa Mkoa wa Kaskazini Pemba
alisema, hatokuwa tayari kuona fedha za miradi hazitumiwi ipasavyo.
Alisema kuwa, fedha
ambazo zinazotolewa kwa ajili ya miradi ya maendeleo ikiwa hazikutumika kwa
mujibu wa utaratibu huathiri sana, hivyo aliwataka wasimamizi kuwa makini na
wawe na tabia ya kuelekezana na kushauriana, ili fedha zitumike kwa usahihi.
“Fedha zilizotumika
kujengea uwanja huu haziendani kabisa na hadhi ya kiwanja kilivyo, ipo haja kwa
wote wanaohusika kusimamia ipasavyo miradi inayowafikia na fedha zitumike kama
ilivyokusudiwa”, alisema Mkuu huyo.
Aidha Mkuu huyo
alisema, awali alielekeza kwamba katika kiwanja hicho kujengwe sehemu za kukalia
watu wanaokwenda kuangalia michezo sambamba na kupandwa miti ya kivuli,
ingawa yote hayo hayakufanyika.
“Lengo letu ni
kuimarisha vijana kwa kuonesha na kukuza vipaji vyao, hii itasaidia kuzalisha
ajira miongozi mwa ajira laki tatu zinazotakiwa kutoka katika sekta rasmi na
zisizo rasmi”, alieleza.
Alieleza kuwa, kwa
sasa ipo haja ya kuandaa makundi madogo madogo ili yaweze kucheza ligi ndogo
ndogo sambamba na kuweka kiwango japo kidogo cha fedha ambacho watapewa
washindi, jambo ambalo litasaidia kuamsha ari kwa vijana hao katika sekta ya
michezo.
“Kiwanja
kimetengenezwa kwa fedha nyingi, hivyo tuwaandae vijana wakitumie ili tuone
kwamba kinaleta faida kubwa katika mkoa wetu”, alieleza.
Mapema Ofisa Mdhamini
Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Salum Ubwa Nassor alisema, Ilani
ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015/2020 iliahidi kujenga viwanja vya michezo
kisiwani Pemba kwa lengo la kuisaidia kuimarisha miundombinu ya viwanja na
kupewa fursa ya michezo mbali mbali kuanzia ngazi ya shehia, Wilaya na Mkoa.
Alisema kuwa, taarifa
ya utekelezaji katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali imetenga shilingi
milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa viwanja viwili vya Wilaya, ambapo kwa Pemba
wamefanikiwa kujenga Kishindeni Wilaya ya Micheweni na Kangani Wilaya ya
Mkoani.
“Viwanja hivi
vimejengwa na mkandarasi wa ndani na kwa hatua ya awali vimeshakamilika kwa
mujibu wa makubaliano ya mkataba na kukabidhiwa kwa wakuu wa Wilaya husika na
viko tayari kutumika kwa wananchi”, alisema Mdhamini huyo.
Akizungumzia changamoto
katika uwanja huo alisema, eneo lipo kwenye makaazi ya watu kidogo jambo ambalo
linakosa kutumiwa ipasavyo, hivyo ipo haja kwa wakuu wa Wilaya kuwahamasisha
vijana kwenda kuutumia sambamba na Wizara kuihamasisha ZFA kuutumia.
“Changamoto nyengine
ni kukosekana kwa miundombinu ya kuingilia uwanjani ambayo ipo nje ya uwezo
wetu, wakati wa mvua huwa panajaa maji na watu kushindwa kufika”, alieleza.
Nae Mkuu wa Wilaya ya
Micheweni Mgeni Khatib Yahya alisema kuwa watachukua juhudi mbali mbali
kuhakikisha vijana wanakitumia kiwanja hicho kwa maslahi yao na Taifa kwa
ujumla.
Ziara hiyo ya siku
moja ikiongozwa na Mkuu wa Mkoa kaskazini Pemba Salama Mbarouk Khatib walikagua
miradi mbali mbali ya kimaendeleo na kuwataka wasimamizi wa miradi hiyo kutumia
fedha hizo kama inavyotakiwa.

0 Comments:
Post a Comment