Raya Hamad – OMKR.
Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa
Kwanza wa Rais Dkt Omar. D Shajak amelishukuru shirika la Umoja wa Mataifa
linaloshughulikia idadi ya watu duniani UNFPA kwa juhudi inazozichukuwa katika
kusaidia Watu wenye Ulemavu.
Ameeleza hayo ofisini kwake
Migombani alipofanya mazungumzo na Msaidizi Mwakilishi mkaazi wa UNFPA Dkt
Wilfred Ochan kuhusiana na nafasi ya Watu wenye Ulemavu katika maendeleo ya
nchi na kutoa shukurani kwa shirika hilo kwa kusaidia kuanzisha mfumo jumuishi
wa Watu wenye Ulemavu.
Dkt Shajak amesema kuwepo kwa mfumo
jumuishi wa Watu wenye Ulemavu umekuwa ni suluhisho katika kuisaidia Serikali
kufanya maamuzi sahihi kwa vile unawezesha kujua idadi ya Watu wenye Ulemavu,
aina ya ulemavu wao na kiwango chake pamoja na mahitaji yao.
Amesema mfumo jumuishi unaweka
takwimu sahihi kufahamu ukubwa na udogo wa mahitaji ya Watu wenye Ulemavu na
hatimae serikali kufanya maamuzi mazuri katika ya utekelezaji wa mipango yake
kuanzia ngazi ya shehia hadi serikali kuu.
Aidha amesema pamoja na kuwepo kwa
mfumo huo lakini bado unahitaji maboresho ili uweze kwenda mbali hivyo kupitia
UNFPA anaimani wataweza kufikia malengo na watu wenye Ulemavu kupata stahiki
zao zote ikiwemo kuwajengea uwezo kielimu, afya na ushiriki wao katika masuala
ya maendeleo ya kiuchumi.
Nae Msaidizi Mwakilishi mkaazi wa
UNFPA Dkt Wilfred Ochan amesifu jitihada zinazochukuliwa na Serikali ya
Mapinduzi Zanzibar kupitia Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais kwa juhudi
wanazozichukuwa katika kuwasaidia Watu Wenye Ulemavu.
Amesisitiza umuhimu wa kuhakikisha
masuala ya Watu wenye Ulemavu yanaendelea kutambuliwa na kuingizwa katika sera
kwenye sekta mbali mbali kama vile afya, elimu, miundombinu shirikishi, makaazi
na ajira ilikuwepo na ufanisi.
Kupitia UNFPA wameahidi kuendelea
kufanya kazi na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais kupitia Baraza la Watu wenye
Ulemavu na kuona namna ya kufanya mashauriano katika mpango mkuu wa miaka
mitano ujao ili kuyaingiza masuala ya Watu wenye Ulemavu yakiwemo masuala ya
afya ya uzazi na kuwajengea uwezo kielimu. .


0 Comments:
Post a Comment