Na Salum Vuai
MWANDISHI wa habari wa Idhaa ya
Kiswahili katika Shirika la Utangazaji la Uingereza BBC Zuhura Yunus, amezindua
kitabu alichoandika kutambua mchango wa wanawake katika kufanikisha Mapinduzi
ya Januari 12, 1964 visiwani Zanzibar.
Katika uzinduzi wa kitabu hicho uliofanyika Novemba 6,
2021 kwenye hoteli ya Golden Tulip iliyoko karibu na uwanja wa ndege Zanzibar,
mwanahabari huyo Mtanzania mwenye asili ya Zanzibar, alitaja mambo kadhaa
yaliyomtia shauku ya kuandika riwaya hiyo adimu.
Alisema kitabu hicho alichokipa jina la ‘Biubwa Amour
Zahor: Mwanamapinduzi mwanamke’, kimelenga kuonesha ushiriki wa wanawake ambao
kwa bahati mbaya hautajwi inavyostahiki katika kuwakumbuka watu waliofanikisha
Mapinduzi yaliyoung’oa utawala wa kigeni hapa Zanzibar na kuwapa wazalendo
uhuru wa kujitawala.
Alisema maudhui ya riwaya hiyo yalikusanywa kutoka kwa
watu mbalimbali ndani na nje ya Tanzania wanaomjua Biubwa Amour Zahor ambaye
ndie muhusika mkuu.
“Azma yangu ni kutaka kufuta dhana iliyoganda katika
akili za watu wengi kwamba wanawake wa Kizanzibari eti ni ‘legelege’, na kuonesha
namna Biubwa alivyoendesha harakati na kuwa kiungo muhimu kwa waasisi wa
Mapinduzi hayo,” alisema mtangazaji huyo maarufu wa BBC Swahili.
Alieleza kuwa inasikitisha kwamba wakati Mapinduzi
hayo yakikaribia miaka 58 sasa, mchango wa wanawake umekuwa
ukisahaulika, na pale unapokumbukwa hautajwi kwa ukubwa wake halisi.
“Tukio hili muhimu katika historia ya Zanzibar limekuwa likionekana kama ni
la wanaume tu, wanawake waliokuwa mstari wa mbele katika
mapambano ya kuuangusha utawala wa kigeni wanapewa nafasi ndogo sana kwenye maandishi ya
historia ya tukio hilo au hawapewi kabisa,” alibainisha.
Zuhura aliishauri Serikali ya Mapinduzi Zanzibar
kuzijumuisha kumbukumbu zinazowaelezea akinamama majasiri walioshiriki kwa
namna tofauti harakati za siasa hadi kufanyika Mapinduzi, na kuziweka katika
makumbusho ya ‘Mapinduzi Square’ Michezani na majengo mengine ya
kihistoria ili nao wafahamike.
Mgeni rasmi
katika uzinduzi huo Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Dk. Saada Mkuya Salum, aliusifu ujasiri wa
muhusika mkuu Biubwa, kwa kuridhia kuelezea namna alivyozijua na
kushiriki harakati za Mapinduzi akitoa kila aina ya msaada kwa washiriki
wanaume hadi yakafanikiwa.
Aidha, alimpongeza Zuhura Yunus, kwa jitihada zake
ambazo alisema zimeinua hadhi ya mwanamke wa Kizanzibari na kuiongezea thamani
historia ya visiwa hivi kwa kuonesha ukweli uliokosa sauti.
“Hii simulizi ya mwanamke aliyesimamia kile
alichokiamini, iwe chachu ya kuamsha ari kwa wengine kufanya tafiti na kuandika
vitabu vingi zaidi kuhusu utajiri mkubwa wa historia na maudhui mengine kuhusu
Zanzibar ambavyo vinaweza kutumika kufundishia katika skuli zetu,” alieleza
Waziri Mkuya.
“Sehemu ambayo
ilinigusa sana na kunitoa
machozi niliposoma kitabu hiki, ni suala la unyanyasaji wa kijinsia. Kumbe mambo haya yalikuwepo tokea zamani. Ila ujasiri wa Biubwa
kumsimulia Zuhura
naye akaweza kuandika si kitu kidogo,” alisema.
Kwa upande mwengine, Dk. Mkuya alieleza kuwa kitabu hicho kinaonesha pia umuhimu wa elimu kwa wanawake wa
Kizanzibari na nguvu walizonazo iwapo wanapewa nafasi na kuongeza
kuwa, kama angelipata fursa ya kukipa jina jengine, angekiita ‘Nguvu ya Mwanamke.’
Kitabu hicho ambacho Zuhura alianza kukusanya maudhui
yake tokea mwaka 2017, kinatarajiwa kuzinduliwa pia jijini Dar es Salaam
Novemba 13, 2021, na kinapatikana kwa nakala ngumu na laini.
Jumla ya nakala 150 ziliuzwa wakati wa hafla ya kukizindua
iliyohudhuriwa pia na mawaziri mbalimbali wastaafu na wa sasa, watendaji wa
taasisi za umma na binafsi pamoja na mabalozi kadhaa.
Wengine ni wadau wa fasihi na uandishi, familia ya
mtunzi na muhusika mkuu Biubwa Amour Zahor, na uhakiki wake ulisomwa na
mwanaharakati Salma
Maoulid, huku kikundi cha Tausi Women Taarab na Rahat zaman
vikitoa burudani mwanana ya taarab asilia.

0 Comments:
Post a Comment