| Picha sio halisia |
Salum Vuai
HUKU tukiwa katika wiki ya maadhimisho ya afya ya
akili duniani, jamii inapaswa kutafakari ili kujua kwa kiasi gani inatimiza
wajibu wake katika kuwatunza ndugu zetu wanaokabiliwa na tatizo hilo.
Kwanza ni lazima tufahamu kwamba maadhimisho hayo
yanayofikia kilele Oktoba 10, hayakuanzishwa kuwa ni sherehe ya kujifurahisha,
kama inavyofanyika kwenye mambo mengine mathalan siku ya uhuru au ile inayoitwa
ya wapendanao (Valentine Day).
Bila shaka hii ni siku maalum kwetu kufanya tathmini
ya pamoja juu ya changamoto zinazowakabili wenzetu wanaopatwa na fadhaa ya
kurukwa na akili hata mara nyengine wakafanya mambo yasiyostahili kutendwa na
mtu mwenye akili timamu na tena kadamnasi.
Ni vyema jamii ifahamu kwamba kamwe hakuna mtu
anayependa kuwa mgonjwa wa afya ya akili, bali yote yanayomkuta ni kwa kudra na
mipango ya Mwenyezi Mungu.
Katika miaka ya nyuma, watu wengi walijenga tabia
mbaya ya kuwachokoza ndugu zetu wenye maradhi hayo huku wakiwapachika majina
mengi mabaya.
Majina kama vile chizi, kichaa, mwehu, punguwani,
mwendawazimu na mfano wa hayo, yalikuwa ndiyo wapewayo jambo ambalo ni
unyanyapaa uliokithiri.
Kwa kuwa wenzetu hawa ni binadamu, tabaan
wanapochokozwa huchokozeka na wengine hawahimili na hivyo huonesha hasira zao
kwa kuokota mawe na kuwarushia hao wasiokuwa na utu, imani wala kuthamini haki
ya wagonjwa hao.
Lakini ni jambo zuri kwamba kitengo cha afya ya akili
katika hospitali ya Kidongochekundu, kimefanya kazi nzuri kutoa elimu kwa jamii
ili itambue kuwa hao ni wagonjwa wanaohitaji mapenzi na kutunzwa badala ya
kugeuzwa karagosi mitaani.
Lolote utakalolifanya dhidi ya mtu mwenye tatizo la
afya ya akili ambalo lina namna nyingi tofauti, ni vyema ukumbuke usemi,
“Hujafa hujaumbika”.
Kwa kuwa hakuna aijuaye kesho yake, ili mradi yuko hai
basi lolote linaweza kutokea, na si ajabu kupata maradhi yoyote ikiwemo ya
akili kwa namna moja au nyengine ile ijapo isiwe kiasi cha kupiga au kugombana
na watu ovyo.
Pamoja na kazi nzuri inayofanywa na hospitali ya
Kidongochekundu na Wizara yote ya Afya, bado wapo baadhi ya watu wanaendeleza
vitendo vya unyanyapaa kwa wagonjwa wa afya ya akili.
Katika tafakuri ya leo, Muhenga ameamua kuwapa elimu
watu wanaopenda kuwakebehi ndugu zetu wenye mtindio wa ubongo maarufu sura
mfanano kila wanapowakuta mitaani.
Yumkini huko ndiko kuonesha mapenzi kwao kwa
kuwashirikisha katika baraza na michezo yao, lakini mara nyengine huwageuza
watu wa kufurahisha jamii katika njia ya uchale.
Inashangaza mara kadhaa utakutana nao mitaani
wakiwaimbisha nyimbo na kuwataka wanengue, huku wao wakifurahia kwa kupiga kofi
na kuangusha vicheko.
Baya zaidi, wanapofanya hayo, huwa wameshughulika
kurekodi kwa simu zao kisha kusambaza video hizo katika makundi ya ‘Whatssap’
na marafiki zao mbalimbali.
Je, wafanyao haya kwa watoto wa wenzao, wana uhakika
gani kwamba nao au jamaa zao hawatakuja kuzaa watoto wenye kasoro za maumbile
mbalimbali ikiwemo ya aina hiyo?
Hatuombi yatokee, lakini hata wao wenyewe, wanadhani
hawawezi kutokezewa na mabadiliko ya kiakili kutokana na sababu mbalimbali
ikiwemo kuchanganyikiwa kimaisha?
Tuelewe kwamba Mwenyezi Mungu ndie muweza wa yote,
hivyo kila analolifanya kwa binadamu ni miongoni mwa mitihani yake kwetu ambayo
inahitaji subira, imani na mafunzo kwa wengine.
Wakati tukiungana na nchi nyengine duniani kuadhimisha
siku ya afya ya akili, tukumbuke kwamba sote ni wagonjwa watarajiwa wa maradhi
yoyote yale, hivyo tusikufuru kwa kuyaona matatizo ya wenzetu wengine kuwa ni
komedi ya kufurahisha nyoyo zetu kwani kwa Mungu hakuna kubwa.
Mwisho lakini si kwa umuhimu, Muhenga anachukua fursa
hii kuwapongeza madaktari, wauguzi na wataalamu wote katika vitengo vya afya ya
akili Unguja na Pemba kwa juhudi zao za kuwashughulikia ndugu zetu wanaopata
matatizo hayo.
Aidha, kazi kubwa wanayofanya kutoa elimu ili
kubadilisha mitazamo hasi iliyomo katika jamii zetu, na kuwezesha kupungua sana
vitendo vya kuwanyanyapaa ndugu zetu hao.
Kama bado wapo wanaoendeleza unyanyapaa watu wenye
tatizo la afya ya akili, ninaamini kwa tafakuri hii watakuwa wamejifunza na
nitarajie kutoka sasa nao watakuwa walimu wazuri kwa wengine.
SIMU: 0777865050/0714 425556
Baruapepe: salumss@yahoo.co.uk
0 Comments:
Post a Comment