| Bandari Bubu |
WAFANYABIASHARA
kisiwani Pemba wametakiwa kuacha tabia ya kuingiza bidhaa kwa njia ya magendo
kwani wanaikosesha Serikali mapato yake ambayo husaidia kutumika kwenye miradi
ya maendeeo.
Akizungumza na
mwandishi wa habari hizi Mdhamini wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwa
upande wa Pemba Habib Saleh Sultan alisema, wafanyabiashara waelewe kwamba
fedha zinazokusanywa ndizo zinazojengewa vituo vya afya, skuli, kuwafikishia
wananchi huduma za umeme, maji safi na salama na huduma nyengine.
Alisema kuwa, kuna
baadhi ya wafanyabiashara hutumia bandari bubu kuingiza bidhaa kwa lengo la
kukwepa kodi, jambo ambalo sio sahihi, kwani mapato yanayokusanywa na Mamlaka
ndio yanayowanufaisha wananchi kutokana na huduma za kijamii wanazofikishiwa.
Alieleza kuwa, pamoja
na vikosi vya ulinzi na usalama vinavyofanya doria katika maeneo ya bahari,
lakini wafanyabiashara wamekuwa wakitumia njia mbali mbali ambazo huingiza
bidhaa bila kuonekana, hali ambayo inawapa wakati mgumu katika kutekeleza
majukumu yao ya kukusanya Kodi.
“Kuna vikosi vya ulinzi
na usalama lakini binadamu hawezekani, na wala hawaogopi kwa sababu akikamatwa
tunataifisha bidhaa na chombo kilichobeba hatimae kupata wao hasara kwani ni
lazima walipe faini, ila hawajali”, alisema Mdhamini huyo.
Alisema kuwa, wamekuwa
wakifanya jitihada mbali mbali kuhakikisha wanaondosha kadhia hiyo ili Serikali
ipate mapato yake, ingawa sio kitu rahsi, hivyo wanaendelea kutoa elimu kwa
wananchi, jambo ambalo wanaamini litawasaidia kutataua changamoto mbali mbali
katika ukusanyaji wa mapato.
“Tumekuwa tukitoa elimu
kwa wananchi, wafanyabiasha wadogo na wakubwa pamoja na wanafunzi wa skuli za Chasasa
Wete, Madungu na Fidel Castro Chake Chake na Uweleni Mkoani ambazo zimo kwenye
mradi maalumu”, alisema.
Alifahamisha kuwa, Serikali
ya awamu ya nane kupitia Dk, Mwinyi inawajali wananchi wake katika mambo mbali
mbali, ambapo kupitia kodi inajaribu kufanya kila hali kuona kwamba wanaweza
kulipa kodi.
Alieleza kuwa, pamoja
na kwamba Serikali inahitaji fedha kwa ajili ya kufanya shughuli zake za
kimaendeleo, lakini kuna vitu ambavyo imeona kuwa, ipo haja ya kuhakikisha viwango
vya kodi vinamsababishia mfanyabiashara kumrahisishia kulipa kodi yake.
“Kuna bidhaa mbali
mbali ambazo kwa sasa zimeondolewa ushuru na zile ambazo ni za wafanyabiashara
wadogo wadogo ambao wanaonekana kwamba kipato chao ni kidogo, hivyo tuone umuhimu
huu wa Serikali kutujali”, alifafanua.
Akizungumzia changamoto
nyengine zinazowakabili katika ukusanyaji wa mapato alisema, ni wafanyabiashara
kutokuweka kumbu kumbu katika mauzo yao, jambo ambalo linaifanya Mamlaka
ikadirie.
“Ikiwa wanaweka kumbu
kumbu zao vizuri inakuwa rahisi kujua mauzo ya mfanyabiashara, lakini kama hana
risiti ni lazima tumkadirie na hapo ndipo kunatokea malalamiko ya wafanyabiashara”,
alisema Mdhamini huyo.
Aidha aliwataka
wafanyabiashara hao kushirikiana pamoja na TRA ili kujua utaratibu mzima wa
kulipa kodi, sambamba na kuijua sheria ya kodi, kwani itawasaidia kufahamu kitu
ambacho anastahiki kulipa.
Kwa upande wao
wafanyabiashara wamesema kuwa wamekuwa wakiweka kumbu kumbu wanapouza bidhaa
zao, ingawa kwa Pemba hakuna mzunguko wa biashara kutokana na kuwa bei za
bidhaa ni kubwa.
“Bidhaa inapofika Pemba
huwa tushalipia kodi sehemu nyingi, hivyo hatuwezi kuuza bidhaa kwa bei ndogo
jambo ambalo linasababisha wateja kufika kwa uchache”, walieleza.
Walisema kuwa, wafanyabiashara
wanaweza kukaa dukani kuanzia asubuhi hadi anapoondoka hajauza chochote na ndio
maana wakati mwengine wanashindwa kulipa kodi, kwani kipato chao kinakuwa
kidogo.
Ili Serikali ipate
mapato yake na kufanya miradi mbali mbali ya kimaendeleo ambayo huwanufaisha
wananchi, ipo haja kwa wafanyabiashara kulipa kodi kwa wakati sambamba na
wananchi kudai risiti wakati wanaponunua bidhaa.
0 Comments:
Post a Comment