NA ZUHURA
JUMA, PEMBA
JESHI la
Polisi Mkoa wa Kaskazini Pemba limesema, litaendelea kupambana na
udhalilishaji, ili kuhakikisha vitendo hivyo vya kikatili vinaondoka katika
Mkoa wao.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi Ofisini
kwake Wete, Kamanda wa Polisi Mkoa huo RPC Juma Sadi Khamis alisema, hawatokuwa
tayari kuona watoto wanadhalilishwa huku watendaji wa makosa hayo wakidunda
mitaani.
Alisema kuwa, Jeshi la Polisi litaendelea kuchukua
juhudi mbali mbali za kupambana na vitendo vya udhalilishaji, kwa kuwachukulia
hatua stahiki watendaji wa makosa hayo, ili kuhakikisha kila mmoja anaogopa.
“Ni vyema kabisa wananchi kuacha tabia hizi za
udhalilishaji ambazo zinakwenda kinyume na sheria na yeyote atakaefanya hivyo
tutaendelea kupambana nae kwa lengo la kuondosha kabisa vitendo hivyo”,
alisema.
Alieleza kuwa, wanawake na watoto wanahitaji
kuheshimiwa, kuthaminiwa na kutunzwa, jambo ambalo litasaidia kupata vizazi
vilivyo bora na vyenye kufuata maadili mema.
Kamanda Sadi alieleza kuwa, wamejipanga ipasavyo
kuona jamii inaishi kwa salama, kwani wananchi tayari wameshapata elimu ya
kutosha juu ya mambo ya udhalilishaji, hivyo yamepungua kwa kiasi fulani.
“Tunashukuru wananchi wameelewa kutokana na elimu
wanayopewa, matukio yamepungua kiasi, tunatumai kumaliza kabisa”, alisema
Kamanda huyo.
Hata hivyo aliwataka wananchi kuacha tabia ambazo
ziko nje ya maadili, kwani Zanzibar inafuata maadili mema ambayo husaidia
kuipeleka jamii pahala pazuri.
0 Comments:
Post a Comment