NA
WAANDISHI WETU, PEMBA
MAHAKAMA
ya Mkoa B Chake Chake imemuhukumu mganga wa kienyeji kwenda kutumikia chuo cha
mafunzo kwa muda wa miaka 30 na kumlipa muathiriwa fidia ya shilingi milioni
moja, baada ya kupatikana na hatia ya kumbaka mke wa rafiki yake.
Mganga huyo aliejulikana kwa jina Issa Abdalla
Haji mwenye umri wa miaka 41 mkaazi wa Wawi Chake Chake, amehukumiwa kifungo
hicho mara tu baada ya kukubali kosa hilo.
Akisomewa shitaka lake na wakili wa Serikali
kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa mashitaka Ali Amour Makame, mshitakiwa huyo
alikubali kutenda kosa hilo na kuiomba mahakama impunguzie adhabu.
“Mshitakiwa
ulimbaka mwanamke baada ya kumuaminisha kwamba wewe ni mganga wa
kienyeji utakaemfanyia dawa ya kumtoa mume wako ambae yupo rumande
anaeshitakiwa katika kesi ya jinai namba 140/2021, kosa la wizi wa kutumia silaha, jambo ambalo
ni kosa kisheria”, alidai mwendesha mashitaka.
Hakimu wa Mahakama hiyo Luciano Makoye Nyengo,
baada ya mshitakiwa kukubali kosa lake, alimuamuru kwenda chuo cha mafunzo kwa muda
wa miaka 30 na kumlipa muathiriwa fidia ya shilingi milioni moja.
Kwa mujibu wa maelezo ya hakimu huyo, mshitakiwa
alikuwa rumande na rafiki yake, ikiwa yeye anakabiliwa na tuhuma za wizi huku
rafiki yake akikabiliwa na tuhuma za wizi wa kutumia silaha.
“Walipokuwa rumande rafiki yake alimwambia kwamba,
amwambie mke wake akamchukulie dhamana ili na yeye akitoka akamwambie mke wake
akamchukulie dhamana”, alisema hakimu huyo.
Alisema kuwa, baada ya mganga huyo kupata dhamana,
alikwenda moja kwa moja kwa mke wa rafiki yake na kumwambia akamchukulie mumewe
dhamana huku akimpa masharti ya uganga.
“Alimwambia ili mume wako apewe dhamana, lete nywele
za sehemu za siri za mbele pamoja na mbegu za kiume, akimaanisha wafanye
mapenzi ili wapate hizo mbegu za kiume”, alisema Hakimu.
Kwa mujibu wa hati ya mashitaka ya mshitakiwa huyo
alitenda kosa hilo Oktoba 11 mwaka huu
saa 12:00 jioni Wawi Chake Chake, bila ya halali alimbaka mwanamke baada ya
kumuaminisha kwamba atamfanyia dawa ya kumtoa mume wake ambae yupo rumande.
Kufanya hivyo ni kosa kinyume na kifungu cha
108(1), (3),(d), na 109(1) sheria ya adhabu, sheria nambari 6 ya mwaka 2018,
sheria ya Zanzibar.
0 Comments:
Post a Comment