Wenye ulemavu Pemba walia na utowaji wa huduma ya chanjo ya Corona

Muonekano wa mji wa Chakechake mkoa wa kusini Pemba



Baadhi ya watu wenye ulemavu wilaya ya Chake chake, wamependekeza kuwa, kituo cha chanjo dhidi ya UVIKO 19, kiondolewe kilipo sasa, kwenye jengo la ghorofa moja la Hospitali ya Chake chae, na kishushwe chini ili kuwarahisishiya wanaotaka huduma hizo.

Walisema, kwa watu wenye ulemavu na hasa wa viungo na macho, imekuwa tatizo kuzifikia huduma za chanjo na kusababisha usumbufu kwao.

Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi, walisema kwa wenzao wenye ulemavu kama miguu na macho ni tatizo wanapotaka huduma hiyo.

Mmoja kati ya watu wa kundi hilo, Amiri Haji Amiri mwenye ulemavu wa viungo, alisema hakuna hata mmoja wao anaweza kufizifikia huduma za chanjo, zilizopo hospitali ya Chake chake.

Alisema, kwa vile pana ngazi mbili kabla ya kuzifikia, inaweza kuwa kikawazo chengine kwao, kuzifikia huduma hizo ambazo nao ni haki yao kiafya.

“Ni vyema mamlaka husika kuangalia kuzihamisha huduma za chanjo hospitali ya Chake chake, maana ziko juu na sisi wengine hali yetu ni ya ulemvu, inatubidi tubebwe,’’alieleza.

Khadija Hassan Omar, alisema wakati mumefika kwa tasisi hasa za umma, kuzingatia majengo rafiki kwa kundi la watu wenye ulemavu, wawe sawa na wengine.

Alieleza kuwa, mfano wa huduma hizo za chanjo ni jambo moja, ingawa zipo huduma nyingine, katika ofisi za umma nazo watendaji wako juu.

“Unakuta jengo linaghorofa zaidi ya moja, kisha hakuna ngazi mwendo ‘lift’ na pengine msemaji kuu ndio amechangua chumba kilichoko juu, hii sio haki kwetu,’’alilalamika.

Mjumbe kutoka Umoja wa watu wenye ulemavu Zanzibar ‘UWZ’ ofisi ya Pemba Hidaya Mjaka Ali, alisema suala la chanjo ya UVIKO -19 ni haki ya makundi yote.

Alieleza kuwa, ili kufikia hilo, ni vyema kwa wizara ya Afya kuzingatia jengo na eneo zinapotolewa, ili zisiwe chanzo cha ugumu kwa kundi la watu wenye ulemavu.

Akizungumzia hilo, Mratibu wa maradhi yanayoambukiza Pemba Khamis Bilali, alisema kwanza kutokana na miundimbinu ya jengo lao, kwasasa ni vigumu kulibadilisha.

Alisema utaratibu wao ni kuwafuata wenye mahitaji maalum kwa kushuka madakatari chini na kuwapatia huduma za chanjo, iwe ni wenye ulemavu au wagonjwa wengine.

“Ni kweli kwa sasa eneo ambalo tumeliteua kwa ajili ya chanjo UVIKO-19, ndani ya hospitali ya Chake chake, inabidi mwenye kuhitajia apandishe ngazi mbili, lakini akiwa hawezi madaktari wanamfuata alipo.

Katika hatua nyingine, Mratibu huyo alisema, kama kundi la watu wenye ulemavu na wameshajikusanya pahala, Idara yake itawafuata kuwapa huduma hiyo popote walipo.

“Chamsingi wajikusanye na kuwasiliana na sisi Idara ya chanjo, watu hao wenye ulemavu au mahitaji maalum, ili wasipate usumbufu, bali sisi ndio tutawafuata hata kama visiwani,’’alifafanua.

Hata hivyo aliwataka wananchi kuendelea kuitumia fursa hiyo ya chanjo na hasa kwa vile ni bure, na waondoe dhana iliyopo kuwa chanjo hiyo ni hatari kwao.

“Jamani serikali yetu inawapeda mno watu wake, hivyo kweli ipokee chanjo ambayo inaathari, na kisha iwatake hata madaktari wake wachome chanjo hii,’’alifafanua.

Zoezi la uzinduzi wa chanjo ya UVIKO -19 kwa kisiwani Pemba lilizinduliwa rasmi Augosti 27, mwaka huu katika hospitali za Micheweni, Wete, Mkoani na Chake chake Pemba.

 

 

 


 

About mmedia

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 Comments:

Post a Comment