Na Salum Vuai
TAARIFA ya
wafadhili wa mradi unaolenga kuwarudisha skuli watoto wa Zanzibar
walioacha masomo kwa sababu mbalimbali kwamba bado idadi ya wanawake ni ndogo,
inahitaji kukaliwa kitako na kufanyiwa kazi.
Wakati Zanzibar
chini ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali ikiwa katika hekaheka za
maadhimisho ya Elimu bila Malipo, ni jambo la faraja kuwa shughuli hiyo
inakwenda sambamba na mradi wa kuwarudisha skuli watoto walioko nje ya
madarasa.
Kwa namna ya
pekee, kupitia tafakuri hii Muhenga analipongeza Shirika la UNICEF pamoja na
taasisi inayoshughulikia masuala la elimu kwa wote, EAC kutoka nchini Qatar kwa
kuleta mradi huo wa miaka mitatu hapa Zanzibar.
Sio siri kuwa
tunao vijana wengi waliolazimika kukatisha masomo kwa sababu mbalimbali na
wazazi au walezi wao kushindwa kuwahimiza, lakini sasa wanajuta na kutamani
kuipata tena nafasi waliyokuwa wameipoteza.
Hata
hivyo, pamoja na kazi nzuri inayofanywa na Wizara kuhakikisha mradi
huo unafanikiwa kikamilifu, iko haja kwa jamii, wazazi na walezi
wa watoto husika kuona umuhimu wa fursa hiyo na kuitumia ipasavyo.
Mradi huo
unaolenga kuwafikia wanafunzi 35,732 katika wilaya zote Unguja na Pemba, ni
fursa adhimu inayopasa kupokelewa kwa mikono miwili na wazazi pamoja na vijana
wenyewe kujikubalisha kurudi skuli ingawa wengine wameshakuwa wakubwa.
Taarifa za
Wizara ya Elimu zinaeleza kuwa zaidi ya wanawake 16,000 kati ya idadi
iliyotajwa, ni miongoni mwao, lakini kasi yao ya kurudi hadi sasa imekuwa ya
kusuasua.
Ni kweli kwamba
kwa maumbile yake, mtoto wa kike akikatisha masomo na kupita muda mrefu akiwa
nje, pengine wazazi wamempa mume na Mungu akamjaalia mtoto/watoto, suala la
kurudi skuli kwake linakuwa gumu.
Akirudi darasani
ambako kuna mchanganyiko wa wanafunzi wa umri tafauti wanaoangaliwa uwezo wao
kabla kutawanywa kwenye madarasa mengine mbalimbali kulingana na umri na
ufahamu wao, mwanamke anaweza kuona aibu hasa akiwa amezungukwa na watoto
wadogo.
Tuwaambie umri
usiwe kikwazo, kwani hata wazee wetu waliokosa elimu kabla ya Mapinduzi,
baadae walikuwa wakisoma madarasa ya jioni yaliyokuwa yakiendeshwa
katika matawi ya Chama cha Afro Shirazi (ASP) kabla ya kuungana na TANU cha
Tanzania Bara Febuari 1977 kuunda CCM.
Elimu hiyo ya
watu wazima, angalau wajue kusoma, kuandika na kuhesabu.
Aidha, katika
kuwatengenezea fursa za kujiendeleza vijana walioacha masomo kabla kuhitimu
elimu ya lazima, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imeunda Idara ya Elimu Mbadala
ili kuwapa taaluma na stadi mbalimbali za maisha inayoweza kuwasaidia kuajirika
au kujiajiri wanapohitimu.
Jamii yote
inapaswa kuunganisha nguvu ili kuhakikisha kati ya vijana wote 35,732
waliolengwa na mradi huu, hakuna anayeachwa nyuma awe mwanamme au mwanamke.
Na inapohusu
wanawake, hata taasisi za kiraia na wanaharakati wanaoshughulikia ustawi wa
vijana na wanawake, waangalie namna wanavyoweza kutoa mchango wao katika
kuwasukuma wanawake wasione aibu kurudi skuli.
Taasisi kama
TAMWA, BIWO, ZAFELA na jumuiya zote za vijana, ziungane kuisaidia
Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kuwahamasisha watoto wetu kurudi masomoni.
Katika hili,
ninawapongeza wafadhili wa mradi huu pamoja na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya
Amali, kwa ubunifu wao wa kuwapatia nyenzo na vifaa vyote vinavyohitajika
vijana wanaorudi skuli ili kuwaongezea hamu ya kubaki madarasani na kusoma.
Inafurahisha
kuwa, mbali na vifaa vya kujifundishia darasani, pia wanapewa vifaa
vya michezo kwa kadiri wanavyohitaji ili kuwazoesha mazingira ya kurudi kuwa
wanafunzi, ambayo walikwisha kuyasahau.
Kwa namna hii,
ninaamini lengo litafikiwa na mradi utakapomalizika mwaka 2023, sote tutajumuika
kufurahia matunda yake.
Kwa maoni na ushauri
0777 865050/0714
425556

0 Comments:
Post a Comment