![]() |
Makamu wa kwanza
wa rais wa Zanzibar Othman Masoud Othman akizungumza na Mabalozi wa
Tanzania walioteuliwa hivi karibuni. Kulia kwa Mhe. Makamu ni Balozi wa
Tanzania nchi Itali Mhe. Mahmoud Thabiti Kombo na Balozi wa Tanzania nchini
Uturuki Luteni Genrali Y. H. Mohammed.
Mabalozi hao walifika ofisini kwa makamu Migombani kubadilishana mawazo pamoja
na kumuaga kuelekea kwenye vituo vyao vya kazi. ( Mpiga Picha Maalum)
MAKAMU wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Othman Masoud
Othman, amesema changamoto inayoikabili Tanzania, kama ilivyo kwa nchi nyingine
za Afrika, ni kuchelewa kutumia fursa kupitia Jumuiya na Taasisi za Kimataifa
katika kujiletea maendeleo.
Othman aliyasema hayo leo
Ofisini kwake Migombani Jijini hapa, alipokutana na Mabalozi sita waliofika
kujitambulisha na kumuaga kabla ya kuelekea vituo vyao vya kazi, katika Mataifa
mbali mbali, ndani na nje ya Afrika.
Alisema zipo fursa nyingi muhimu kupitia jumuiya na taasisi
mbali mbali za kimataifa, zikiwemo za kujiletea maendeleo na kujikwamua, bali
ushiriki wa Tanzania na Afrika kwa ujumla ni mchache, au hakuna kabisa, na
inabaki kuwa changamoto.
Othman ambaye aliwahi kuwa Mwakilishi wa Afrika katika Shirika
la Umoja wa Mataifa linalohusiana na Haki Miliki (‘World Intellectual Property
Organization’ (WIPO), amebainisha fursa hizo kuwa ni pamoja na maendeleo ya
teknolojia, ushindani wa kibiashara na uwekezaji.
“Naelewa changamoto kubwa iliyopo, lakini ni vyema tukaelewa
kuwa kwa sasa ulimwengu hauelekezi nguvu zake zaidi upande wa mapambano ya
kijeshi, bali vita kubwa iliyopo ni ya teknolojia katika kuhamasisha maendeleo
ya kiuchumi”, alisema Othman.
Makamu huyo aliwanasihi Mabalozi hao kuzidi kujitolea na kutumia
kila juhudi katika kujenga mahusiano mema yatakayowezesha kuibua fursa ambazo
kwa kiasi kikubwa zinahitajika katika jamii pamoja na serikali za mitaa, na
wala siyo katika kujikita kujenga mahusiano na Serikali Kuu pekee.
“licha ya kuwatakia kila la heri katika utekelezaji wao wa
majukumu, ameeleza imani yake kwa Mabalozi hao akiamini kuwa mafanikio yao
ndiyo heshima ya nchi, na pia kufanikiwa kwa Taifa hili na watu wake” alieleza
Othman.
Naye Kiongozi wa Kundi la Mabalozi hao, Mahmoud Thabit Kombo,
aliyeteuliwa kuwa Balozi wa Tanzania nchini Italy, ameeleza changamoto ya
vikwazo vya mawasiliano katika uzoefu wa kidiplomasia, hali inayokwaza azma ya
miradi ya maendeleo na inayowakatisha tamaa baadhi ya wawekezaji.
Balozi Mahmoud ameahidi kuwa yeye na wenzake watajitahidi kwa
hali na mali kuzikabili changamoto hizo, na hawatosita kuomba msaada kupata
busara kutoka kwa Othman kila inapobidi, ili kuzichuma fursa katika Mataifa wanayokwenda
kuiwakilisha Tanzania, kwaajili ya maendeleo ya nchi na Taifa kwa ujumla.
Wengine katika kundi la Mabalozi hao na vituo vyao vya kazi ni
pamoja na Meja Jenerali Richard Makanzo (Rwanda), Hoyce Anderson Temu
(Switzerland), Grace Alfred Olotu (Sweden), Elsie Sia Kanza (Marekani) na
Luteni Jenerali Mohamed Yussuf (Uturuki).
Waliojumuika na ujumbe huo ni pamoja Mkurugenzi wa Mambo ya Nje
wa Zanzibar, Balozi Masoud Abdalla Balozi.

0 Comments:
Post a Comment