![]() |
| Makamu wa kwanza Othman Masoud Othman akifungua Kongamano la walimu katika ukumbi wa Idrisa Abdul wakili Kikwajuni Zanzibar |
MAKAMU wa Kwanza wa
Rais Zanzibar, Othman Masoud Othman, amesema kwamba ni muhimu kwa walimu
kujengewa uwezo zaidi ili kuwa sambamba na mahitaji ya elimu yanayokwenda na
kasi ya mabadiliko ya dunia.
Makamu ameyasema
hayo leo, alipofungua kongamano la walimu huko katika Ukumbi wa Sheikh Idrissa
Abdul-wakil Kikwajuni mjini Zanzibar, ikiwa ni matayarisho ya kuelekea kilele
cha Siku ya Walimu Duniani inayoadhimishwa tarehe 5 Oktoba, ya kila mwaka.
Akizungumzia hadhi
ya walimu hapa Zanzibar, Othman amesema imeshuka na kuitaka jamii na hasa walimu kuweka mikakati ya suluhisho la vikwazo
katika maendeleo ya elimu .
Kuhusu maslahi ya
walimu, Mhe. Othman amesema serikali inaendelea na juhudi za kuleta mageuzi ya
elimu na suala hilo linasubiri idhini ya serikali ili hatua zaidi kuchukuliwa.
Aidha kuhusu mapambano
dhidi ya unyanyasaji wa watoto, amewataka walimu kushirikiana na Polisi,
Wanasheria na Mawakili kuandaa mkakati shirikishi utakaongoza na kusimamia
vyema mapambano dhidi ya tatizo hilo.
Kuhusu haki za walimu Makamu ameshauri kutumia utaratibu
wa majadiliano baina ya walimu na
serikali ambayo ni kazi isiyo na gharama kwa kusaidia kujenga mfumo utakachangia
kuondosha matatizo yao.
Naye Waziri wa Elimu na
Mafunzo ya Amali Zanzibar Simai Mohammed Said, amesema serikali kupitia
wizara hiyo inakaribisha kuwepo majadiliano na waalimu ili kutafuta ufumbuzi wa
changamoto zinazoikabili sekta hiyo.
Katika risala yao iliyosomwa na Mwalimu Haji Juma Omar, wameipongeza Serikali kutokana na juhudi kubwa za kutia moyo zinazofanywa katika maendeleo ya sekta ya elimu pamoja na kuendeleza maridhiano ya serikali ya Umoja wa kitaifa
Hata hivyo, wametanabahisha
serikali kufahamu kwamba, skuli nyingi zinakabiliwa na changamoto za
kimazingira ikiwa ni pamoja na kukosekana hati miliki na kusababisha maeneo
mengi kuvamiwa kwa shughuli za ujenzi wa makaazi.

0 Comments:
Post a Comment