TUFUATENI MIONGOZO YA DINI ILI KUIRUDISHA HADHI YA ZANZIBAR - ALHAJ OTHMAN MASOUD
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Alhaj Othman Masoud Othman, amewasihi Waislamu nchini kurudi katika mila, desturi na kufuata sheria za dini ili kutunza haiba na sifa za Zanzibar kote ulimwenguni.
Ameyasema hayo mara baada ya kumaliza ibada ya Sala ya Ijumaa katika Masjid Shifaa uliopo Michenzani Mjini Unguja, ambapo amesisitiza kuwa kuna mambo mengi yaliyokuwa yakifanywa na wazee wetu walioishi nchini zikiwemo mila na desturi zinazoendana na miongozo ya dini ya Kiislamu ambayo yaliipa heshima kubwa Zanzibar.
“Zamani wageni waliokuwa wakitembelea hapa walikuwa wakiishi kupitia mila na silka zetu na hilo ndilo lililoifanya Zanzibar kupata umaarufu”, amesema akiongeza kwamba hayo ni mambo ya kudumishwa ili Zanzibar irudi katika hadhi na haiba yake.
Alhaj Othman amekumbusha kuwa hapa Zanzibar kuna mambo mengi yamefanywa na watawala wa Kiingereza kama vile kuanzisha mahakama ya kadhi, kamisheni ya wakfu na kuongoza nchi kwa sheria ya Kiislamu kutokana na kukuta kuwa nchi hii ilikuwa na misingi ya dini na mila bora kabisa.
"Kama tutafuata vyema miongozo ya dini, basi jamii zetu zitakuwa na upendo na kuheshimiana sana jambo litakaloondoa hata vitendo vya kihalifu" alisisitiza Makamu huyo wa kwanza wa Rais.
Mapema khatibu wa msikiti huo, Sheikh Ahmed Muumin, amewahimiza Waislamu hao kuutumia muda wao katika kufanya amali njema kwa lengo la kujitengenezea maisha bora kwa Mwenyezi Mungu.
0 Comments:
Post a Comment