Zanzibar tunakwama wapi miundombinu isiyohimili mvua?



Na Salum Vuai

MVUA ni neema ambayo kila mja anaihitaji na kama inapita miezi au miaka bila kunyesha, viumbe tunakuwa mashakani.

Mvua huleta maji yanayohitajika kuhuisha ardhi ili mazao yanawiri na kujaza vianzio vya maji hayo ambayo kuwepo kwake ndio furaha ya kila kiumbe.

Si mwanadamu, mnyama, ndege, miti na hata wadudu warukao na kutambaa, anayeweza kuishi kwa raha bila ya maji.

Lakini pamoja na uzuri wake, mvua inaponyesha katika nchi au eneo lisilokuwa na miundombinu rafiki, ni wazi madhara yatatokea na mara nyengine makubwa sana kiasi cha kuporomosha majengo na kuondoka na roho.

Kwa bahati mbaya sana, katika kipindi cha kuanzia miaka ya 1980 hadi sasa, hapa kwetu Zanzibar kila msimu wa mvua unapowadia inakuwa karaha badala ya raha, na nakama badala ya neema.

Lakini la kusikitisha zaidi, Serikali hutumia fedha nyingi kutengeneza miundombinu kwa lengo la kuzuia mafuriko na kutuwama kwa maji katika maeneo ya makaazi na majengo ya ofisi bali tija haionekani.  

Bila shaka maji ni muhimu lakini katu hayafai kufungiwa njia ili mvua inaponyesha  yaweze kupita kwa urahisi na kuwaacha viumbe na makaazi yao salama.

Lakini hivyo sivyo ilivyo hapa nchini, kwani pamoja na watu kuhitaji mvua, inapopatikana inakuwa wasiwasi mtupu wakikumbuka tafrani iliyowakumba misimu iliyotangulia.

Tayari mfano umeonekana kutokana na mvua zilizoanza kunyesha siku tatu zilizopita katika maeneo mengi ya Zanzibar hasa mjini ambako miundombinu haikidhi haja wala kuwahakikishia wananchi usalama wa kutosha.

Katika hali ya kawaida, mvua za awali huonesha mapungufu yaliyopo juu ya paa la nyumba yetu, kwani kila palipo pabovu patavuja na hii inayonyesha sasa imefichua udhaifu wa miundombinu yetu.

Lakini tujiulize, kwa nini iwe tunasubiri mvua zituoneshe matundu badala ya kutumia kipindi cha kiangazi kujiandaaa mapema kukabili athari zinazoweza kujitokeza?

Je, ni yepi matokeo ya miradi ya ujenzi wa miundombinu iliyolenga kudhibiti kutuwama kwa maji ambayo imegharimu mapesa mengi mno, tena mengine ni misaada na mikopo ambayo walipaji ni sisi walipa kodi wanyonge?

Ukiacha udhaifu wa viwango katika misingi na njia za maji, wananchi nao wanafanya makosa sana kuongeza ukubwa wa tatizo.

Khulka ya wakaazi wa maeneo mengi kuigeuza misingi kuwa ndio majaa ya kutupia taka, ni ukosefu wa nadhari na isipoachwa inaweza kutuletaa janga kubwa la mafuriko.

Ifahamike kuwa kutupa taka katika misingi kunaziba njia ambazo zimejengwa ili kusafirisha maji kwenda baharini au sehemu nyengine zilizotengwa kwa ajili hiyo.

Hali kama inayoonekana eneo la posta Kijangwani wakati wa mvua, njia kutuwama maji pamoja na mitaani, ni matokeo ya tabia isiyokuwa ya kistaarabu kutupa taka kila pahala hata misingini.

Lazima jamii ifahamu kwamba uchafu ukichanganyika na maji matokeo yake ni mazalia ya nzi ambao ni wadudu waenezao maradhi hasa ya matumbo na kipindupindu.

Hakuna asiyejua ubaya wa kipindupindu ambacho kikipiga hodi hakiwaachi watu salama na mara nyingi vifo mfululizo na vya haraka huchukua nafasi.

Hali hii ikitokea, inakuwa marufuku hata kuwatembelea wagonjwa wanaotengewa kambi mbali na familia na jamii zao kutokana na tabia ya maradhi hayo kuambukiza kwa kasi.

Ufike wakati tuiweke nchi yetu Zanzibar katika mandhari nzuri ya kuhimili hali zote kiangazi na mvua, ili shughuli ziendelee bila kikwazo chochote.

Serikali ifanye wajibu wake kuhakikisha ujenzi wa miundombinu unakuwa na kiwango kinachoakisi thamani ya fedha zinazotumika, lakini na wananchi nao waitunze na kuilinda isiharibiwe kwa kumwagiwa taka.

Wenye dhamana ya kutoa zabuni kwa wakandarasi wasiweke mbele tamaa binafsi kwa kuchagua washindi kwa upendeleo wakitarajia pasenti kama bahashishi yao.

Pia wakandarasi nao wasifanye ghushi kwa kutumia vifaa duni au kupunguza saruji na kuongeza mchanga, kitendo kinachoweza kutusababishia majuto kwa ubovu wa majengo, misingi na barabara zetu.

Simu: 0777 865050/0714 425556


About mmedia

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 Comments:

Post a Comment