Ndugu waandishi wa habari;
Tumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia kuwa katika hali ya
uzima, afya bora na kutuwezesha kufika hapa leo, katika shamra shamra za
shuguli za maadhimisho ya siku ya Kimataifa ya Watu wenye Ulemavu Duniani.
Shukrani za pekee ziwaendee wanahabari wote mliopo hapa kwa kuona umuhimu wa
shughuli yetu hii katika kuifahamisha jamii juu ya siku ya Kimataifa ya Watu
wenye Ulemavu.
Kama inavyoeleweka, ifikapo tarehe 3 Disemba ya kila mwaka
Zanzibar inaungana na nchi nyengine ulimwenguni katika kuadhimisha siku ya
Kimataifa ya Watu wenye Ulemavu Duniani. Maadhimisho hayo yanatufanya tuweze
kutafakari juu ya maendeleo na changamoto mbalimbali walizonazo Watu wenye
Ulemavu ili kufikia Maendeleo Jumuishi kwa wote.
Ndugu waandishi wa habari;
Historia inaonesha kwamba, harakati za kupigania haki na fursa
za Watu wenye Ulemavu zilianza miaka ya 1970 kwa nchi Wanachama katika Umoja wa
Mataifa baada ya kupitia na kuangalia masuala yote yanayohusu maisha na
maendeleo ya watu wote duniani. Hivyo, wameona kuwa, bado masuala ya Watu wenye
Ulemavu hayajatiliwa mkazo wa aina yoyote hasa katika upande wa suala la haki
za kibinadamu.
Hatua mbalimbali zilichukuliwa kwa kipindi cha miaka mingi
kuanzia mwaka 1981, hadi mwaka 1992, maamuzi ya mwisho yalitangazwa tarehe 3
Disemba 1992 kuwa kila ifikapo tarehe 3 Disemba ya kila mwaka iwe ni Siku ya
Kimataifa ya Maadhimisho ya Haki za Watu wenye Ulemavu Duniani, kwa misingi ya
kuhakikisha kwamba, suala la Watu wenye Ulemavu ni moja kati ya masuala
mengineyo ya Haki za Binadamu Duniani
Ndugu waandishi wa habari;
Siku hii imepewa kipaumbele, umuhimu na ulazima wa kuadhimishwa
kila mwaka duniani kote, kwa nchi wanachama zilizoridhia Mkataba wa Kimataifa
wa haki za Watu wenye Ulemavu, kuendena na kauli mbiu ya mwaka huu”
Ndugu waandishi wa habari;
Kwa mujibu wa kauli mbiu ya mwaka huu inayosema “Uongozi na
Ushirikishwaji wa Watu wenye Ulemavu, kuelekea ujumuishwaji na ufikiwaji
endelevu baada ya uviko 19 Duniani”
Uchambuzi na ufafanuzi wa kauli mbiu hii imezingatia masuala
mbali mbali yakiwemo: -
Usawa katika kupata mawasiliano
Mara nyingi Watu wenye Ulemavu katika suala la mawasiliano
wanapata changamoto kubwa ambapo wanakuwa hawawezi kujua katika taifa lao kwa
kila kinachotokea, kwani miundombinu ya huduma hii si rafiki kwao na inapelekea
kukosa huduma mbali mbali katika jamii kwa wakati muafaka.
Kuwawezesha katika kupata maendeleo
Hii inatoa msisitizo wa kauli mbiu ya mwaka huu. Ushirikishwaji
wa Watu wenye Ulemavu, tunakusudia kusema kuwa, Watu wenye Ulemavu wanapaswa
kushirikishwa katika mipango yote ikiwemo ya kisera kwa masuala yanayohusu
kundi hili. Si jambo la busara hata kidogo na haitapendeza iwapo jamii
itawatenga na kuwanyanyapaa kwa kutowashirikisha katika masuala tofauti
yakiwemo hata yale yanayowahusu.
Chombo kikuu cha utendaji kuhusiana na masuala ya Watu wenye
Ulemavu ni Baraza la Taifa la Watu wenye Ulemavu ambalo pamoja na majukumu
yake, Katika kuhakikisha kuwa Watu wenye Ulemavu wanapata maendeleo, kundi hili
liweze kujumuishwa katika nyanja zote zikiwemo za kisiasa, kijamii na
kiuchumi.
Ndugu waandishi wa habari;
Umoja wa Mataifa kupitia viongozi wakuu wa Serikali wa nchi
mbali mbali walishiriki mkutano uliofanyika makao Makuu ya Umoja wa Mataifa
huko Marekani tarehe 24-25 Septemba mwaka huu, katika mkutano huo iliamulika
kwamba ni kuwekwa mkazo katika kufanya mapitio makubwa juu ya utekelezaji wa
malengo 17 ya maendeleo endelevu ifikapo 2030. Sambamba na hayo; Mkutano huo
umepitisha maazimio ya kuboresha zaidi utekelezaji wa agenda iliyoibuliwa mwezi
Septemba 2015 kuwa ifikapo 2030 pamoja na kupitisha azimio la kisiasa.
Kwa mujibu wa kaulimbiu ya mwaka huu inavoeleza kuwa “Uongozi na
Ushirikishwaji wa Watu wenye Ulemavu, kuelekea ujumuishwaji na ufikiwaji
endelevu baada ya uviko 19 Duniani”
Hii ndio kusema kuwa, Watu wenye Ulemavu wana haki ya
kushirikishwa katika nyanja zote za kiuchumi kama raia wengine wote wa nchi hii
bila ya kujali ulemavu wao Kwani tunachoangalia si ulemavu wao bali taunatizama
haki zao na uwezo walionao.
Ndugu waandishi wa habari;
Ndugu waandishi wa habari na washiriki wote kwa ujumla, haki hii
ya kushiriki katika shughuli za kimaendeleo imeelezwa katika Ibara ya 29 ya
Mkataba wa Kimataifa wa Watu wenye Ulemavu ulioridhiwa Tanzania mwaka
2009.
Mkurugenzi wa Baraza la watu wenye Ulemavu Zanzibar Ussy Khamis Debe akifafanua jambo wakati walipotoa taarifa kwa vyombo vya habari kuelekea kuadhimisha siku ya watu wenye ulemavu Duniiani
Ndugu waandishi wa habari;
Toka kuundwa kwa Idara ya Watu wenye Ulemavu, yapo yafanikio
mengi yaliyopatikana, mafanikio hayo ni pamoja na: -
• Kuwepo kwa Mfuko wa Maendeleo ya watu wenye ulemavu, Mfuko
ambao tayari umeeshanza kuwanufaisha walengwa ikiwa ni pamoja na mikopo, msaada
wa kielimu na matibabu. Hali hii imekuwa ni faraja kwa watu wenye ulemavu kwani
umewasaidia kutokana na hali ngumu ya kiuchumi na utegemezi, pia kutokana mkopo
huu kutokua na riba imekua ni jambo la faraja kwa watu wenye ulemavu kwani zipo
taasisi nyingi ambazo zinatoa mikopo lakini ni kikwazo kikubwa kwao kutokana na
hali zao
• Kuwa na takwimu za Watu wenye Ulemavu kupitia usajili na mfumo
wa kielectroniki kwa ajili ya Watu wenye Ulemavu unaojulikana kwa jina la
JUMUISHI DATA BASE hili ni suala la kupigiwa mfano, kwani Serikali yetu imeweza
kutambua idadi ya Watu wenye Ulemavu na mahitaji yao kupitia mfumo huo
ulioanzishwa pamoja na usajili uliofanyika, Aidha taarifa za Watu wenye ulemavu
sasa zinakusanywa kwa njia ya simu (Mobile Aplication). Ukusanyaji mwa taarifa
kwa njia hii umeipunguzia serikali, Gharama ya kutumia karatasi nyingi kwa
ajili ya kukusanyia taarifa vilevile mfumo huu unawezqa kuhesabiwa Mtu mwenye
Ulemavu mara tu ya kumaliza kutoa taarifa zake.
• Kuwepo kwa taarifa ya upembuzi yakinifu juu ya
huduma ya afya ya ya uzazi na uzazi wa mpango kwa vijana wenye ulemavu Unguja
na Pemba.
• Kuwepo kwa Mpango mkakati wa Baraza la Taifa la Watu wenye
Ulemavu (2019 - 2024) ambao utasaidia Baraza kufanyakazi kwa ufanisi zaidi ya
kuishauri Serikali kuhusu masuala ya Watu wenye Ulemavu na kutekeleza mambo
muhimu kwa maendeleo ya Watu wenye Ulemavu.
• Kuwepo kwa marekebisho ya Sera ya Watu wenye Ulemavu ya mwaka
2018 yatakayoenda sambamba na marekebisho ya Sheria au kutungwa Sheria mpya
pamoja na mpango wa utekelezaji wa Sera hiyo ni msingi mzuri utakaowataka wadau
wote kutoa haki kutoka ngazi ya Shehia hadi taifa na kufanya wajibu wao kwa
Watu wenye Ulemavu hapa Zanzibar, sera hiyo imegusa maeneo 10, yakiwemo;
1. Upatikanaji wa huduma kwa Watu wenye Ulemavu,
2. Mifumo ya hifadhi ya jamii,
3. Usimamizi wa majanga,
4. Mazingatio katika ajira,
5. Ufikiaji wa huduma za mawasiliano,
6. Ufikiaji wa huduma za kinga na tiba,
7. Elimu na ushirikishwaji wa watu wenye Ulemavu,
8. Ufikiwaji wa haki za kisheria,
9. Ufikiaji wa Watu wenye Ulemavu katika michezo na burudani na,
10. Elimu, ushirikishwaji na ushiriki wa Watu wenye Ulemavu.
• Kuwepo kwa Maafisa Waratibu wa masuala ya Watu wenye Ulemavu
katika Wizara za Serikali, kuwepo na maafisa walemavu Mkoa na maafisa walemavu
Wilaya wanaosimamia utekelezaji na ushirikishwaji wa Watu wenye Ulemavu katika
masuala mbali mbali kwa mujibu wa ngazi zao.
• Kuanzishwa kwa Kamati za Shehia zitakazoshughulikia masuala ya
Watu wenye Ulemavu katika ngazi za Shehia.
Serikali imeweka muongozo maalum ili maendeleo ya nchi
yetu yasiwaache nyuma Watu wenye
Ulemavu kwa kuboresha muundo wa taasisi wa Watu wenye ulemavu kwa kuanzisha
Maafisa Walemavu Mkoa, Wilaya na Kamati za Shehia, hii inarahisisha kuibua
changamoto mbalimbali za Watu wenye Ulemavu katika ngazi za shehia na serikali
kuweza kuzifanyia kazi kwa haraka changamoto hizo.
• Kuwepo kwa Muongozo wa viwango vya Miundombinu rafiki kwa Watu
wenye Ulemavu.
• Kuwpo kwa mkakati wa ushawishi na mawasiliano wa Watu wenye
Ulemavu
Ndugu waandishi wa habari;
Nitoe shukurani zangu za dhati kwenu waandishi wa habari kwa
kukubali kushirikiana nasi katika kufanikisha masuala mbali mbali ya Watu wenye
Ulemavu likiwemo hili la leo. Aidha, mashirikiano haya ya karibu tunakuombeni
yaweze kudumu zaidi na zaidi.
Mwisho kabisa, nitoe wito kwenu na kukuombeni nyinyi waandishi
wa habari kuwa, muwe mabalozi wazuri katika kuufanyia kazi kwa vitendo kauli
mbiu yetu ya mwaka huu kwani tukifanya hivyo tunaweza kufikia sera ya serikali
ya awamu ya nane ya Uchumi wa Buluu wenye neema na mafanikio mazuri kwa Watu
wenye Ulemavu na Taifa kwa ujumla.
AHSANTENI SANA KWA
KUNISIKILIZA
0 Comments:
Post a Comment