| wavuvi wa WeteMkoa wa kaskazini Pemba |
WAVUVI wa Mkoa wa Kaskazini Pemba wameiomba Serikali ya
Mapinduzi Zanzibar kuwaondolea ushuru kwenye vifaa vyote vya uvuvi, ili dhana
ya uchumi wa buluu iweze kuwanyanyua wao na kuinyanyua Zanzibar kiuchumi.
Walisema kuwa, vifaa vya uvuvi vimekuwa na bei kubwa vinapofika
Zanzibar kutokana na ushuru uliopo, kiasi ambacho wanashindwa kuvinunua na
kusababisha kuvua samaki kidogo ambao hawakidhi mahitaji yao, kwani kipato
kinachopatikana hakiwatoshelezi.
Walisema kuwa, wanaamini kwamba Serikali ya Mapinduzi Zanzibar
inawapenda sana na ndio maana ikaundwa Wizara ya Uchumi wa Buluu, hivyo ipo
haja ya kuondolewa kila changamoto zinazowakabili, ili kuwainua kiuchumi kwani
asilimia kubwa ya wananchi wa Pemba wanategemea rasilimali ya bahari.
"Vifaa tunavyotumianni nyavu, jarife, mishipi, mashine za
boti na vifaa vyengine, lakini kwa hapa kwetu havinunuliki mpaka tuagize
wenyewe kutoka Dubai inakuwa afadhali na kuagiza ni shida sana", walisema
wavuvi hao.
Wakizungumza katika mkutano wa mapendekezo ya rasimu ya Sheria
ya Uvuvi uliofanyika katika Ukumbi wa Baraza la Wawakilishi Wete, wavuvi hao
walipendekeza Sheria ya kuwekewa mahakama yao maalumu, kwani wao sio wahalifu.
"Kwa nini sisi tunapelekwa mahakamani kama wahalifu,
tunataka Sheria ituwekee mahakama yetu maalumu kama ilivyo kwa Baraza la Mji na
sehemu nyengine, pia leseni za uvuvi zitolewe na Wizara ya Uchumi wa Buluu
kwani ndio wanaojua shida zetu na sio SUMATRA", walisema.
Mwenyekiti wa Kamati ya Uvuvi Wilaya ya Wete Mohamed Kombo Hamad
(Mwinyi mpeku) alifahamisha kuwa, Kamati za uvuvi zinahitaji zitambulike
kisheria sambamba na mapato yao kukusanywa na Wizara inayohusika na uchumi wa
buluu na sio Baraza la Mji ama Halmashauri, kwani wanapopata matatizo hata
hawashughuliki.
"Kila siku tunakatwa fedha sio kidogo lakini zinapotokea
matatizo baharini kama ya kupotea ama kuzama kwa boti, tunapigania wenyewe
Baraza hata halitutambui, hivyo hatutaki wakusanye wao maana hazitunufaishi
pesa zetu", alisema Mwinyi Mpeku.
Aidha alisema kuwa, muwekezaji wowote atakaekwenda kuekeza
katika mkondo wa Pemba lazima Kamati zishirikishwe, ili wapate ajira ambazo
zitakuwepo.
Kwa upande wake Bidawa Kassim Haji alieleza kuwa, katika Sheria
mpya ziwepo kanuni na leseni ambazo zitawalinda ndani na nje ya nchi kama
silaha yao, kwani wavuvi wamekuwa wakipata tabu sana juu ya hilo.
Nae Kombo Malik Mbwana alisema, wavuvi wamekuwa wakizaraulika
kiasi ambacho hata zinapotokea ajali hakuna boti za uokozi zinazokwenda
kuwasaidia licha ya fedha ambazo wanakusanya kila siku wanaporudi kuvua.
"Kinachotushangaza ni kule tunapookota boti baharini,
tukishazifikisha juu Serikali inazichukua na kuziuza bila sisi tulohangaika
kutuuliza chochote, hii sio haki kwani tulitakiwa tupewe sisi tuliopata tabu,
lakini sasa tutaziacha waje wachukue wenyewe", alisema.
Mapema akifungua mkutano huo Afisa Mdhamini Wizara ya Uchumi wa
Buluu na Uvuvi dk Salim Mohamed Hamza aliwataka washiriki wa mkutano huo kutoa
mapendekezo ya Sheria ambayo yatasaidia kuboresha zaidi, ili uchumi uwe
endelevu.
"Kama mnavyojua kwamba azma ya Serikali ya awamu ya nane ni
kukuza uchumi katika mazingira ya bahari ili uwe endelevu, hivyo ikiwa Sheria
zitakuwa nzuri, malengo ya Serikali yetu yataweza kufikiwa na wananchi watafaidika",
alifahamisha Mdhamini huyo.
Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Uvuvi Salim Sudi Ame
alieleza kuwa, lengo la kuboresha Sheria hizo ni kwenda mbele kimaendeleo,
hivyo watoe maoni yao ili tume ya irekebishe Sheria hizo, kwani hawataki kuona
kwamba Sheria zinawakwaza wananchi.
Nae Mkurugenzi wa Idara ya Hifadhi alisema kuwa, sehemu kubwa ya
Uchumi wa Zanzibar inategemea bahari, ni vyema wakaitumia fursa hiyo bila
kuharibu rasilimali za bahari, kwani hawatoweza kuzalisha vizuri.
Akiwasilisha mada ya rasimu ya Sheria ya Uvuvi mwanasheria Asha
Mohamed Kombo aliwataka wavuvi hao wasifanye uvuvi haramu ambao huharibu na
badala yake watumie uvuvi wenye tija utawasaidia katika kuwapatia kipato
kitakachowakwamua na maisha duni.
Mkutano huo wa siku moja ulifanyika katika Ukumbi wa Baraza la
Wawakilishi Wete, ambao uliwashirikisha wavuvi na wakulima wa mwani, kwa lengo
la kutoa mapendekezo yao yatakayosaidia kuboresha Sheria mpya.
0 Comments:
Post a Comment