Ili kuyafikia maendeleo ya kweli kuna haja ya kuongoza kwa misingi ya ustaarabu.................. Othman

Mjumbe wa Kamati Kuu wa chama ACTV wazalendo Othmani Masoud Othman akimkabidhi mwananchama mpya kadi ya chama hicho huko Uzini Ng’ambwa Mkoa wa kusini Unguja wakati wa ziara yake maalum ya kuonana na wazee na wafuasi  wa chama hicho.


Baadhi ya Wanachama wapya waliojiunga na chama cha ACT wazalendo wakionyesha kadi zao kijiji cha Uzi Ng’ambwa Mkoa wa Kusini Unguja ambapo zaidi wanachama wapya 50 walijiunga na chama hicho


UNGUJA

MJUMBE wa Kamati Kuu ya Chama cha ACT-Wazalendo, Othman Masoud Othman, amesema ili kuyafikia maendeleo ya kweli, kuna haja ya kuiongoza nchi kwa misingi ya kistaarabu, inayojali matakwa na maslahi ya umma.

 

Othman ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar, ameyasema hayo leo akiongea na wafuasi na wanachama wa chama hicho, wa vijiji vya Uzi na Ng’ambwa, Wilaya ya Kati, Mkoa wa Kusini Unguja.

 

Amesema Zanzibar itaweza kuendelea kwa kuzingatia mfumo bora na makini, unaoheshimu misingi imara ya uongozi, ambayo daima inajali heshima utu wa wananchi wake.

 

Othman ameitaja misingi hiyo kuwa ni pamoja na Katiba inayohitajika sambamba na mfumo bora wa kusimamia na kutekeleza chaguzi huru na za haki, zinazopelekea viongozi waadilifu.

 

“Kinachohitajika ni mfumo uliojengwa na misingi makini ya uongozi na usimamizi wa haki pamoja na uwajibikaji, tukielewa kwamba uchaguzi ndio msingi wa uwajibikaji”, amesema Othman.

 

Aidha amesema heshima ya Zanzibar ni ya tangu zamani, na kwamba ilidhoofika, bali kwa sasa kunahitajika ari, ujasiri na uvumilivu wa hali ya juu kuitetea, kuipigania na kuirejesha.

 

Ametolea mifano nchi za Singapore na Sychelles zilizosonga mbele kimaendeleo na zinazowiana na visiwa vya Unguja na Pemba kijeografia, huku akitaja heshima ya Zanzibar katika mahusiano ya mwanzoni kabisa ya kidiplomasia ambapo Mataifa Marekani na Uingereza yalitanguliza Balozi zao hapa katika miaka ya 1837 na 1841. 

 

Amesema pamoja na mambo mengine yakiwemo uzuri na utajiri wa asili uliojengeka kwa mila, silka na utamaduni bora, lakini visiwa vya Unguja na Pemba vimejaa raslimali muhimu, bali zinazowanufaisha wageni, huku wananchi wengi wakiendelea kuteseka na maisha duni.

 

Pia Othman ameeleza nia ya Serikali ya Awamu ya Nane kukabiliana na changamoto zinazowakabili wananchi wa kisiwa cha Uzi, zikiwemo ukosefu wa barabara, pembejeo za kilimo, bei isiyokidhi ya zao la mwani, na mapungufu katika huduma za kijamii ambazo ni pamoja na elimu na afya.

 

 

Mheshimiwa Othman ametoa wito kwa wananchi kuendelea kushirikiana na kuungamkono juhudi za kujenga misingi ya Serikali ya Umoja wa Kitaifa ya Zanzibar, chini ya maridhiano ya kisiasa ambayo ni alama ya imani na amani, ili kuiendeleza nchi.

 

Akijibu baadhi ya hoja za wananchi juu ya changamoto zinazowakabili, Waziri wa Biashara na Maendeleo ya Viwanda Zanzibar Omar Said Shaaban, amesema Wizara yake inaandaa mazingira ya kuwaendeleza wananchi hao, kwa kuhakikisha kunakuwepo mipango ya kuwapatia unafuu pamoja na juhudi za kuongeza bei na ubora wa zao la mwani linalolimwa kwa wingi kisiwani humo.

 

Awali baadhi ya wananchi wameeleza changamoto zinazowakabili na kubainisha namna walivyochoshwa na ahadi za muda mrefu za kuwapatia huduma muhimu zikiwemo za ujenzi wa barabara inayokiunganisha kisiwa hicho, ambazo wamedai hadi sasa hazijatekelezwa.

 

“Tumechoka kujenga barabara kwa mikono, na hiki ni kilio chetu cha muda mrefu kwa kila kiongozi anayekuja lakini bado hatujapatiwa ufumbuzi”, alisema Bi Fatma Mussa wa Uzi-Mwanzo, akiwasilisha changamoto ambayo imekaririwa pia na Bi Masika Mansab wa Uzi Ng’ambwa mbele ya Mheshimiwa Othman alipoongea na wazee wa kisiwa hicho.

 

Ziara hiyo imemjumuisha Mjumbe wa Kamati Kuu ya ACT-Wazalendo, Ismail Jussa Ladhu ambaye amewataka wananachama na wafuasi wa chama hicho kuendelea na msimamo thabit wa kupigania hadi kufanikisha mamlaka kamili ya Zanzibar bila ya kutetereka.

 

Viongozi mbali mbali walijumuika katika ziara hiyo ambao ni pamoja na Kaimu Naibu Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo Zanzibar, Salim Abdalla Bimani, Wakurugenzi, Wenyeviti wa Mikoa na Wajumbe wa Kamati Kuu ya Chama hicho.

 

About mmedia

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 Comments:

Post a Comment