WAKULIMA wa
kilimo cha mchaichai kisiwani Pemba wamelalamika shirika la Biashara la ZSTC
kuwashushia bei ya mafuta ya mchaichai, licha ya kuwa soko la bidhaa hiyo liko
pale pale.
Wakizungumza na
waandishi wa habari wakulima hao walisema, kinachowashangaza ni kwamba soko la
mafuta ya mchaichai halijashuka, ingawa wakulima wameshushiwa bei kutoka
200,000 hadi kufikia 120,000 jambo ambalo limewatia hasara kubwa.
Walisema kuwa,
ipo haja kwa ZSTC kuwaangalia kwa jicho la huruma wakulima hao, kwani wamekuwa
wakifanya kazi kubwa huku wakiajiri vijana wa kuwasaidia, ingawa kwa sasa
wameshindwa kurudisha hasara na kushindwa kuwalipa wasaidizi.
“Kwa kweli
tumeingiwa wa ugonjwa wa shinikizo la damu (presha) kwa sababu tumeajiri vijana
ili tuwalipe baada ya mavuno lakini matokeo yake kwa bei tuliyopangiwa kuwauzia
ZSTC hatupati kulipa gharama tulizotumia na wala hazikidhi kuwalipa vijana hao,
ni mtihani kwetu”, walisema wakulima hao.
Walieleza kuwa,
katika soko la kimataifa lita moja ya mafuta ya mchaichai wananunua shilingi
320,000 ingawa shirika linanunua kwao kwa shilingi 120,000 jambo ambalo
linawatia unyonge, kwani wao ndio wanaofanya kazi kubwa.
“Mwanzo shirika
lilikuwa linanunua kwetu lita moja kwa shilingi laki mbili na wao wanapata
faida ya 120,000, lakini kinachotushangaza wamekuja kutushushia bei na wala
soko halijashusha bei, hivyo tumepata hasara kubwa na tunadaiwa”, walifafanua.
Mmoja wa
wakulima hao Khamis Ramadhan Faraji mwenye shamba lake Mbiji Mkoani alisema,
walihamasishwa kulima mchachai, ingawa kwa sasa wameanza kuwavunja moyo
kutokana na bei waliyowekewa.
“Sisi ndio
tunaofanya kazi kubwa, tunawalipa watu watusaidie lakini kinachotushangaza na
kutusikitisha ni kuona shirika wanachukua wao pesa kubwa kuliko sisi wakulima,
hii sio haki kutokana na kuwa soko la bidhaa hiyo halijashuka”, alisema mzee
huyo.
Alisema, shamba
lake lina ukumbwa wa ekari tatu na nusu ambalo huzalisha mafuta mengi baada ya
mavuno, ila kinachowasikitisha ni wameanza kuvuliwa matumaini waliyokuwa nayo
kutokana na zao hilo.
“Watu ambao
niliwaajiri kunisaidia katika shamba langu walinishitaki na kunipeleka
mahakamani kwa sababu niliwapa kiwango ambacho hakikufika makubaliano,
niliwambia kwamba bei imeshuka lakini hawakunielewa, kwa kweli nilidhalilika
mtu mzima”, alielezea.
Aidha alisema,
kwa sasa kiwanda ambacho kilikuwa kinawasaidia kukamulia mafuta hayo
kimeharibika, jambo ambalo linawarejesha nyuma zaidi kiutendaji, hivyo aliiomba
Serikali kuwatengenezea ili kuondokana na changamoto hiyo.
Salma Said
Rashid mkulima wa shamba la mchaichai Chonga Wilaya ya Chake Chake alisema,
wamekuwa wakipata hasara kutokana na kushuka kwa bei na kukosekana kwa kiwanda
cha kukamulia mafuta hayo.
“Tunapata shida
wakati tunapotaka kupeleka mchaichai wetu kiwandani, kwa sababu tukipeleka
kiwanda cha Mgelema muhusika mkuu anatwambia kiwanda chake ni cha kukamulia
majani ya mkarafuu na sio mchaichai na kule Mtakata mafuta hayatoki kwani
nyungu zao ni mbovu,” alisema.
Alisema kuwa, walikuwa
wanapata faida wao na wananchi wengine, kwani wakinunua mchaimcha katika maeneo
tofauti ili kuwasaidia kukuza kipato chao, ingawa kwa sasa wanashindwa.
“Kwa kweli
wananchi wengi ilikuwa wanafaidia za bidhaa hii, kwa sababu licha ya kulima
sisi pia ilikuwa tunanunua kutoka kwa wakulima wadogo wadogo angalau na wao
wakipata kujikwamu kimaisha, lakini kutokana na bei ilivyo sasa tumeshindwa
kununua”, alisema Salma.
Asha Juma Rihan
mkulima wa mchaichai katika shamba lenye ukubwa wa ekari saba (7) Pujini Pemba
alisema, hadi kukamilisha upandaji wa bidhaa hiyo ametumia takribani shilingi
milioni 2,000,000.
“Gharama ya
ushughulikiaji bidhaa hii ni kubwa sana, mara zote natumia gharama zaidi ya
milioni mbili lakini ilikuwa napata faida ila kwa sasa hata gharama hatupati
kuzilipa, pia kinachotuumiza zaidi walisubiri tushakamua ndipo wakatushushia
bei, hivyo tuliowaajiri hawajui hilo”, alisema.
Hata hivyo,
ameiomba serikali kuwaongezea bei wakulima wa mchaichai ili kuimarisha na
kuwatia nguvu wakulima wa zao hilo, sambamba na kujipatia faida ambayo
itasaidia kuondokana na umasikini.
Mkurungezi
Muendeshaji wa Shirika la Biashara Zanzibar la ZSTC Said Seif alisema, shirika
lina ulazima wa kununua mafuta ya karafuu na vitu vitokanavyo na karafuu na sio
ya mimea mengine, hivyo ikiwa kuna sehemu wanahisi watapata pesa za ziada
wakauze midhaa yao.
“Sisi tunanunua
pale tunapokuwa na uhitaji na huwa tunauza ujazo mdogo mdogo katika soko la
ndani na sio la kidunia, kwa hiyo mkulima ana hiari yake kwenda kuuza ambapo
anajua atapata bei kubwa, hawajakatazwa”, alisema.
Alisema kuwa,
mafuta ya mchaichai sio ambayo yana soko kidunia ni tofauti na mafuta mengine,
hivyo hulisababishia shirika kupata hasara kila mwaka, kwani ununuliwaji wake
ni wa kusuasua.
“Iyo bei ya laki
tatu sijui wameipatia wapi kwa sababu sisi tunauza kwenye vichupa na sio kwa
ujazo huo wanaosema wao, hivyo wanavyosema sio sahihi hata kidogo”, alisema
Mkurugenzi huyo.
Hata hivyo
Mkurugenzi huyo hakuainisha bei halisi ya kununua mafuta hayo kwa wakulima na
kusema kwamba wao huuza kwa soko la ndani kwa ujazo wa vichupa vidogo vidogo na
sio ujazo mkubwa.

0 Comments:
Post a Comment