Issa
Mzee - Maelezo
Katibu
Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk, Joseph
Edward Sokoine, amesema ushiriki wa Tanzania katika Jumuiya ya nchi zilizopo
kwenye mwambao wa Bahari ya Hindi, unasaidia kikamilifu katika kuzitangaza
fursa za kiuchumi nchini.
Alitoa
kauli hiyo wakati akifungua kikao cha wadau wa nchi zilizopo kwenye mwambao wa
bahari ya hindi, kilichofanyika katika ofisi za ZURA Mjini Unguja.
Balozi
Sokoine, amesema lengo la kuweka kikao hicho ni kukuza uelewa kuhusu majukumu
na ushiriki wa Tanzania katika jumuiya hiyo, ili kuweza kuzitambua na kuzitumia
fursa mbalimbali za kiuchumi kwa maendeleo ya taifa.
Alisema
malengo na majukumu makuu ya jumuiya hiyo ni pamoja na kulinda na kuimarisha
ulinzi na usalama wa bahari, kuimarisha uwekezaji ili kukuza uchumi, kukuza na
kuendeleza sekta ya utalii na utamaduni.
Pia,
kukabiliana na majanga hususan kwenye ukanda wa bahari ya hindi, kuendeleza na
kuimarisha ushirikiano katika uchumi wa buluu pamoja na kuimarisha sekta ya
uvuvi hasa kwenye eneo la bahari kuu.
Katika
kutekeleza majukumu hayo, Dk. Sokoine alisema jumuiya imeunda vikundi kazi ili
kufanikisha na kutekeleza majukumu mbalimbali katika jumuiya hiyo.
Alifafanuwa
kuwa, vikundi kazi hivyo ni vyema vizingatie ushiriki wa pande zote mbili za
Tanzania Bara na Zanzibar ili kuhakikisha ufanisi unapatikana katika kutekeleza
majukumu.
Aidha,
aliwataka wadau kutoa msukumo na kuzipa
kipaumbele shughuli zinazoratibiwa na jumuiya hiyo, ili kujua yanayojiri kwa
lengo la kulinda kwa vitendo maslahi ya Tanzania.
Alieleza
kuwa uanachama wa Tanzania katika jumuiya hiyo ni muhimu katika kuimarisha
uhusiano na mataifa mbalimbali duniani
ambao unatoa fursa ya kubadilishana uzoefu na kuibua changamoto za maendeleo.
Alisema
mada zilizoandaliwa katika kikao hicho zina umuhimu mkubwa na kuleta dira na muongozo katika kutangaza
fursa na rasilimali zilizopo kwenye
ukanda wa bahari ya Hindi.
Vilevile
aliwataka wajumbe hao kutoa mapendekezo yatakayowezesha utekelezaji wa masuala
mbalimbali ya uchumi wa buluu na uhifadhi wa mazingira.
Aidha,
Dk, Sokoine aliwataka wajumbe hao kuomba ufadhili wa miradi ya maendeleo ambayo
italenga zaidi katika uhifadhi wa mazingira pamoja na uvunaji endelevu wa rasilimali za bahari kwa maslahi
ya Tanzania.
Mapema
Mkurugenzi Idara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano
wa Afrika Mashariki Zanzibar, Balozi Masoud Abdalla, alisema utekelezaji wa
sera ya mambo ya nje kwa njia ya amani ni jambo muhimu hasa katika kujadili
faida na fursa za bahari ya Hindi.
Alifahamisha
kuwa, njia ya amani husaidia katika kuimarisha uhusiano wa kimataifa ambao huleta
faida kubwa za kiuchumi ikiwemo muingiliano wa biashara.
Akizungumza
kuhusu uchumi wa buluu, Mkurugenzi huyo alisema sera ya uchumi wa buluu ina
nyenzo kuu tano ikiwemo utalii wa bahari, kilimo cha mwani, bandari, gesi na
mafuta pamoja na uvuvi.
Hata
hivyo alisema umefika wakati wa kutekeleza kwa vitendo sera ya Rais wa Zanzibar,
katika uchumi wa buluu ili kuleta maendeleo nchini.
Kwa
upande wake Mkurugenzi Idara ya Ushirikiano wa kikanda, Balozi Agnes Richard
Kayola, amesema umefika wakati kwa Tanzania wa kuzitazama vyema fursa zilizopo
katika mwambao wa Bahari ya Hindi, ili zitumike kwa maendeleo ya taifa.
Amefahamisha
kuwa, Jumuiya ya nchi zilizopo kwenye ukanda wa Bahari ya Hindi inaundwa na Nchi 23 ikiwemo Tanzania.
Alisema
tangu kuanzishwa kwa jumuiya hiyo, Tanzania haijawahi kugombea nafasi ya Katibu Mkuu, hivyo umefika wakati kwa
Tanzania kugombea nafasi hiyo.
Alisema
kuwa, uimarishwaji wa ushiriki wa Tanzania katika jumuiya hiyo ni muhimu kwa
maslahi mapana ya nchi ambao pia utasaidia katika kukuza uchumi wa bahari
nchini.
Aliongeza
kuwa, uimarishwaji wa vikundi kazi
katika jumuiya hiyo visivyopungua nane, ikiwemo kikundi cha uvuvi, ni jambo
muhimu katika kuimarisha utendaji na kuviunda upya vikundi visivyofanya kazi
vizuri ni jambo la msingi.
Alisema
kikao hicho cha siku tatu kinalengo la kuimarisha ushiriki wa Tanzania kwenye
jumuiya ya nchi zilizopo kwenye mwambao wa bahari ya Hindi.
Katika
kufanikisha hilo, Balozi Kayola amesema ushirikiano wa kisekta baina ya pande
mbili kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi
ya Zanzibar ni muhimu pia ni wa
kuendelezwa.
Katika
kikao hicho mada mbalimbali zilijadiliwa, ikiwemo uchumi wa buluu na tija zake
katika maendeleo ya taifa, uhifadhi wa mazingira na mchango wake katika uchumi
wa buluu, Uvuvi katika bahari kuu, pamoja na fursa za uwekezaji zilizopo kwenye
ukanda wa bahari kuu na Mazao ya Baharini.
0 Comments:
Post a Comment