Ushiriki wa Tanzania katika mwambao wa Bahari unasaia kuitangaza fursa za kiuchumi

   






Issa Mzee  - Maelezo    

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk, Joseph Edward Sokoine, amesema ushiriki wa Tanzania katika Jumuiya ya nchi zilizopo kwenye mwambao wa Bahari ya Hindi, unasaidia kikamilifu katika kuzitangaza fursa za kiuchumi nchini.

Alitoa kauli hiyo wakati akifungua kikao cha wadau wa nchi zilizopo kwenye mwambao wa bahari ya hindi, kilichofanyika katika ofisi za ZURA Mjini Unguja.

Balozi Sokoine, amesema lengo la kuweka kikao hicho ni kukuza uelewa kuhusu majukumu na ushiriki wa Tanzania katika jumuiya hiyo, ili kuweza kuzitambua na kuzitumia fursa mbalimbali za kiuchumi kwa maendeleo ya taifa.

Alisema malengo na majukumu makuu ya jumuiya hiyo ni pamoja na kulinda na kuimarisha ulinzi na usalama wa bahari, kuimarisha uwekezaji ili kukuza uchumi, kukuza na kuendeleza sekta ya utalii na utamaduni.

Pia, kukabiliana na majanga hususan kwenye ukanda wa bahari ya hindi, kuendeleza na kuimarisha ushirikiano katika uchumi wa buluu pamoja na kuimarisha sekta ya uvuvi hasa kwenye eneo la bahari kuu.

Katika kutekeleza majukumu hayo, Dk. Sokoine alisema jumuiya imeunda vikundi kazi ili kufanikisha na kutekeleza majukumu mbalimbali katika jumuiya hiyo.

Alifafanuwa kuwa, vikundi kazi hivyo ni vyema vizingatie ushiriki wa pande zote mbili za Tanzania Bara na Zanzibar ili kuhakikisha ufanisi unapatikana katika kutekeleza majukumu.

Aidha, aliwataka wadau  kutoa msukumo na kuzipa kipaumbele shughuli zinazoratibiwa na jumuiya hiyo, ili kujua yanayojiri kwa lengo la kulinda kwa vitendo maslahi ya Tanzania.

Alieleza kuwa uanachama wa Tanzania katika jumuiya hiyo ni muhimu katika kuimarisha uhusiano na mataifa mbalimbali  duniani ambao unatoa fursa ya kubadilishana uzoefu na kuibua changamoto za maendeleo.

Alisema mada zilizoandaliwa katika kikao hicho zina umuhimu mkubwa na  kuleta dira na muongozo katika kutangaza fursa na rasilimali  zilizopo kwenye ukanda wa bahari ya Hindi.

Vilevile aliwataka wajumbe hao kutoa mapendekezo yatakayowezesha utekelezaji wa masuala mbalimbali ya uchumi wa buluu na uhifadhi wa mazingira.

Aidha, Dk, Sokoine aliwataka wajumbe hao kuomba ufadhili wa miradi ya maendeleo ambayo italenga zaidi katika uhifadhi wa mazingira pamoja na  uvunaji endelevu wa rasilimali za bahari kwa maslahi ya Tanzania.

Mapema Mkurugenzi  Idara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Zanzibar, Balozi Masoud Abdalla, alisema utekelezaji wa sera ya mambo ya nje kwa njia ya amani ni jambo muhimu hasa katika kujadili faida na fursa za bahari ya Hindi.

Alifahamisha kuwa, njia ya amani husaidia katika kuimarisha uhusiano wa kimataifa ambao huleta faida kubwa za kiuchumi ikiwemo muingiliano wa biashara.

Akizungumza kuhusu uchumi wa buluu, Mkurugenzi huyo alisema sera ya uchumi wa buluu ina nyenzo kuu tano ikiwemo utalii wa bahari, kilimo cha mwani, bandari, gesi na mafuta pamoja na uvuvi.

Hata hivyo alisema umefika wakati wa kutekeleza kwa vitendo sera ya Rais wa Zanzibar, katika uchumi wa buluu ili kuleta maendeleo nchini.

Kwa upande wake Mkurugenzi Idara ya Ushirikiano wa kikanda, Balozi Agnes Richard Kayola, amesema umefika wakati kwa Tanzania wa kuzitazama vyema fursa zilizopo katika mwambao wa Bahari ya Hindi, ili zitumike kwa maendeleo ya taifa.

Amefahamisha kuwa, Jumuiya ya nchi zilizopo kwenye ukanda wa Bahari ya Hindi  inaundwa na Nchi 23 ikiwemo Tanzania.

Alisema tangu kuanzishwa kwa jumuiya hiyo, Tanzania haijawahi kugombea nafasi ya  Katibu Mkuu, hivyo umefika wakati kwa Tanzania kugombea nafasi hiyo.

Alisema kuwa, uimarishwaji wa ushiriki wa Tanzania katika jumuiya hiyo ni muhimu kwa maslahi mapana ya nchi ambao pia utasaidia katika kukuza uchumi wa bahari nchini.

Aliongeza kuwa, uimarishwaji wa vikundi  kazi katika jumuiya hiyo visivyopungua nane, ikiwemo kikundi cha uvuvi, ni jambo muhimu katika kuimarisha utendaji na kuviunda upya vikundi visivyofanya kazi vizuri ni jambo la msingi.

Alisema kikao hicho cha siku tatu kinalengo la kuimarisha ushiriki wa Tanzania kwenye jumuiya ya nchi zilizopo kwenye mwambao wa bahari ya Hindi.

Katika kufanikisha hilo, Balozi Kayola amesema ushirikiano wa kisekta baina ya pande mbili kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya  Zanzibar ni muhimu pia ni wa kuendelezwa.

Katika kikao hicho mada mbalimbali zilijadiliwa, ikiwemo uchumi wa buluu na tija zake katika maendeleo ya taifa, uhifadhi wa mazingira na mchango wake katika uchumi wa buluu, Uvuvi katika bahari kuu, pamoja na fursa za uwekezaji zilizopo kwenye ukanda wa bahari kuu na Mazao ya Baharini.

About mmedia

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 Comments:

Post a Comment