Jumla ya hoja kumi na moja zimeondolewa rasmi katika orodha ya hoja za Muungano na kutiwa saini na Mawaziri wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.
Hafla ya utiaji saini wa hati za makubaliano ya kuondoa hoja za Muungano zilizopatiwa ufumbuzi ilifanyika katika ukumbi wa chuo cha utalii Maruhubi nje kidogo ya Mji wa Zanzibar baina ya Mawaziri wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.
Kati ya hoja kumi na moja zilizopatiwa ufumbuzi hoja tisa zimesainiwa hati za makubaliano na hoja mbili ambazo hazihitaji hati za makubaliano tayari zimepatiwa ufumbuzi wa kuitendaji.
Hoja zilizosainiwa hati za makubaliano ni pamoja na uvuvi kwenye ukanda wa bahari kuu, uingizwaji wa maziwa kutoka Zanzibar, ajira kwa watumishi wa Zanzibar katika taasisi za Muungano, mgawanyo wa mapato yatokanayo na misaada kutoka nje.
Pia Mgawanyo wa mapato yatokanayo na misaada kutoka nje, Mkataba wa mkopo wa mradi wa ukarabati wa hospitali ya Mnazi Mmoja, Mkataba wa mkopo wa ujenzi wa barabara ya Chakechake hadi Wete Pemba.
Hoja nyengine ni Mkataba wa mkopo kwa ajili ya ujenzi wa bandari ya Mpigaduri, Usimamizi wa ukokotoaji na ukusanyaji wa kodi kwenye huduma za simu unaofanywa na bodi ya mapato ya Zanzibar na Mapato yanayokusanywa na uhamiaji kwa upande wa Zanzibar.
Akizungumza mara baada ya kukamilika zoezi la utiaji saini Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Philip Isdor Mpango amesema ufumbuzi uliopatikana katika hoja hizo unalenga katika kuhakikisha maslahi ya pande zote mbili yanapatikana ili kuimarisha Muungano.
Alisema tukio hilo ni la kihistoria na muhimu kwa mustakabali wa Muungano na uthibitisho tosha unaothibitisha kuwa kamati inafanya kazi vizuri kwa kuhakikisha Muungano unaleta maslahi pande zote mbili.
“Maslahi ya wananchi wa pande zote Zanzibar na Tanzania bara ni muhimu na yanaendelea kuzingatiwa ni vyema wananchi waelewe ya kwamba serikali zote mbili zipo pamoja kwa maslahi ya wananchi wote” alisema Dk. Mpango.
Alifafanua kuwa kamati imeweza kuzifanyika kazi hoja kumi na moja za muungano ndani ya miaka miwili kutokana na ushirikiano na msingi mzuri ulioekwa na Rais wa Tanzania mama Samia Suluhu Hassan alipokuwa makamu wa Rais.
Dk.Mpango alieleza kuwa faida nyingi zitaweza kupatikana, kutokana utiaji saini wa uvuvi kwenye ukanda wa uchumi wa bahari kuu ikiwemo kupatikana kwa wawekezaji katika sekta ya uchumi wa buluu, na kuongeza ufanisi katika sekta ya uvuvi, na ajira kwa watumishi wa Zanzibar katika taasisi za Muungano utasaidia kuongeza hamasa kwa wananchi katika kupunguza uhaba wa ajira.
Aliendelea kwa kusema, mgawanyo mzuri wa mapato utakaofanyika baina ya pande mbili za Muungano, utasaidia katika kufanikisha miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo miundombinu, pamoja na kuimarika kwa huduma za afya kutokana na marekebisho ya mkataba wa mkopo wa mradi wa ukarabati wa hospitali ya Mnazi Mmoja inayohudumia wananchi mbalimbali nchini.
Aidha alisema huduma za jamii zitaimarika kwa wananchi kutokana marekebisho mazuri ya mkataba wa mkopo wa ujenzi wa barabara ya Chakechake hadi Wete, pamoja na kuiweka Nchi salama kutokana na hatua nzuri iliyochukuliwa katika mkataba wa mkopo wa ujenzi wa Bandari ya Mpigaduri kwa maslahi ya kuzilinda mali za Taifa.
“Nia na madhumuni ya kufanyika hayo yote ni kuuenzi na kulinda Muungano na kuendeleza udugu uliopo”, alisema Dk.Mpango/
Alisema kuwa hoja nyingi zilizokamilishwa zinahusiana na Wizara za Fedha, kwa pande zote mbili za Muungano, na kuwataka Mawaziri wenye dhamana ya Wizara hizo kuzidi kukaa pamoja na kushirikiana katika hatua mbalimbali za kiutendaji.
Vilevile alisema hoja zote zilizobaki zinaendelea kutafutiwa ufumbuzi kwa utaratibu mzuri kwa manufaaa ya pande zote mbili za muungano.
Alitoa rai kwa taasisi zote zinazohusika kuwa, hoja zote zitafutiwe ufumbuzi na hoja zinazojitokeza zijadiliwe kwa uwazi na umakini mkubwa ili kuimarisha Muungano.
Nae Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Hemed Suleiman Abdullah amesema utiaji saini wa hati za hoja za makubaliano ya kuondoa hoja za Muungano zilizopatiwa ufumbuzi baina ya Serikali mbili ni matokeo chanya ya makubaliano yaliyofanywa na Serikali hizo.
Alisema makubaliano hayo yana umuhimu mkubwa kwa maslahi ya Taifa ili kuepusha migongano kwa kizazi cha sasa na kizazi cha baadae .
Alieleza kuwa ufumbuzi uliopatikana utawawezesha wafanyabiashara kufanya biashara zao vizuri bila ya usumbufu wowote nchini.
Aliongeza kwa kusema, tukio hili litasaidia katika kuwajenga wananchi imani kwamba Serikali zao zinafuatilia vyema masuala yote yanayohusu Muungano.
Aidha alitumia fursa hiyo kuwapongeza Mawaziri na Makatibu wote kwa kazi kubwa walioifanya kwa maslahi ya Taifa.
Kwa upande wake Waziri Mkuu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa, alisema upembuzi na mapitio ya hoja zilizopatiwa ufumbuzi ni miongoni mwa kazi kubwa iliyofanywa na kamati ya pamoja jambo ambalo ni muhimu kwa maslahi ya watanzania.
Alisema kuwa hoja mbalimbali zimeweza kupatiwa ufumbuzi katika vikao vilivyofanywa ili kuimarisha Muungano hivyo ni vyema wananchi wazithamini jitihada za viongozi wao.
0 Comments:
Post a Comment